Alhamisi, 18 Juni 2015

MIGOGORO KATIKA TAMTHILIYA YA KISWAHILI

MIGOGORO KATIKA TAMTHILIYA YA KISWAHILI

Katika kazi hii, Istilahi ya tamthiliya  itaelezwa, kisha dhana ya tamthiliya itajadiliwa, historia fupi ya tamthiliya kwa   jumla itaongelewa, historia fupi ya tamthiliya ya Kiswahili, mikondo ya tamthiliya kwa jumla, mikondo ya tamthiliya ya Kiswahili, migogoro katika tamthiliya ya Kiswahili na hatimaye hitimisho.

Tamthiliya ni moja kati ya Tanzu tatu kubwa na muhimu za fasihi. Tanzu nyingine za fasihi ni Ushairi na Riwaya. Tanzu hizi huingiliana. Kwa jumla tofauti kati ya tanzu hizi zimeambatana na malengo na maumbo yake. Mtunzi wa tamthiliya husawiri mawazo kwa maongezi ya wahusika na kwa kujenga migongano na mijadala baina ya wahusika hao. Mshairi hutimia lugha inayonata, lugha inayojirejelea, kwa kufanya hivyo, Mshairi huelezea mapana kwa maneno machache. Mwandishi wa riwaya hujieleza kwa njia ya hadithi hasa akizingatia matukio wanayoyapata wahusika wake.


Dhana hukanganya kwa sababu imeingiliana sana na dhana nyingine kama drama, uigizaji na sanaa ya utendaji. Kama wataalam mbalimbali wanavyofafanua dhana tamthiliya kama ifuatavyo:

 Istilahi “tamthiliya” inatokana na neno “mithali” ambalo lina maana ya “mfano” au ishara ya kitu Fulani. Hivyo katika tamthilya kitu kimoja humithilishwa au huwakilishwa na kitu kingine. Mathalani, katikamchezo wa Kinjeketile, mwigizaji wa sehemu ya “Kinjeketile” huwakilisha mhusika aitwaye Kinjeketile katika mchezo. Hivyo mhusika huyo himithilisha, kwa kiasi Fulani, Kinjeketile wa historia. M.M.Mulokozi,(1996).
Dhana tamthiliya imejadiliwa na wataalam wengi kama ifuatavyo:

Mlama, P(1993:203) anaeleza kuwa tamthiliya ni sanaa ya maonyesho, sanaa ambayo huwasilishwa, ana kwa ana, tukio Fulani kwa hadhira kwa kutumia usanii wa kiutendaji. Kwa mfano, badala ya kuwasilisha wazo kwa hadhira kwa kutumia maneno kama katika ushairi, sanaa za maonyesho hiliweka wazo lile katika hali ya tukio linaloweza kutendeka kwa kutumia usanii wa utendaji kama vile vitendo, uchezaji n.k.

Cuddon,(1979:512) kama alivyonukuliwa na Said A.Mohamed, (1995:59) anaeleza: Tamthiliya ni kazi ya utendaji ambayo hutazamiwa kuonyeshwa jukwaani au redioni au kwenye televisheni, na ambayo matendo yake hufanywa na watendaji wa kike na kiume.

Mulokozi,(1996:188) anafafanua, tamthiliya au drama ni fani ya fasihi iliyokusudiwa kutendwa jukwaani kwa ajili ya hadhira Fulani. Hivyo, lugha ya kawaida, tamthiliya huitwa mchezo wa kuigiza. Tamthiliya huwa na masimulizi ambayo huigizwa na wahusika wa pande mbili au zaidi zinazogongana. Mgogoro huo hatimaye huishia katika mgogoro ambao unaposuluhishwa au kutatuliwa, mchezo huwa umemalizika.

TUKI(2004) nao wanafasili tamthiliya: Ni utungo wa kisanaa ambao huweka wazo Fulani katika matendo na mazungumzo.

Mazrui na Syambo, (1992) wanaelezea tamthiliya: Ni utungo wa fasihi ambao umebuniwa kwa kiasi kikubwa. Kutokana na fasili mbalimbali za tamthiliya, tunaweza kusema kwamba tamthiliya ni aina mojawapo ya sanaa za maonyesho ambayo usanii wa utendaji kama vile ngoma ambazo hutegemea zaidi uchezaji ngoma na upigaji mziki. Tamthiliya ni ule utungo unaweza kuwa umeandikwa au haukuandikwa unaoliweka wazo lilowasilishwa katika umbo la tukio au kuliwezesha kutendeka mbele ya hadhira.

Mhando na Balisidya (1976:83) anasisitiza maelezo hapo kwa kusema : “kigezo kikuu cha tamthiliya ni kuweza kuwasilishwa jukwaani na kutazamwa na hadhira. Tamthiliya huwa na sifa za maonyesho”.

CHIMBUKO LA TAMTHILIYA NA MAENDELEO YAKE KWA UJMLA.

Tamthiliya hupatikana, katika sura mbalimbali duniani kote. Chimbuko lake katika nchi na tamaduni mbalimbali hushabihiana kwa kiasi Fulani kwa vile huhushishwa na visakale na matendo ya kidini.

Tamthiliya ya Ulaya, ambayo ndiyo imeathili zaidi tamthiliya ya Kiswahili, yasemekana kuwa ilitokana na Miviga(rituals) na viviga(rite), hasa ya kidini, katika jamii ya kale ya 
Wayunani. Miviga hiyo iliambatana na dura za kuzaliwa, kukua, kufa, kuoza na kuzaliwa upya ambazo hasa zilihusishwa na Mungu aliyeitwa Dionizi, aliyeaminiwa kuwa aliuawa, akakatwakatwa vipande vipande na baadaye akafufuka tena. Brockett, (1979:4) kama ilivyonukiliwa na Mulokozi, M.M.(1996:190).

Afrika, kumbukumbu za kwanza za maigizo ya kitamthiliya zinapatikana Misri,ambako michezo ya miviga iliyohusu kufa na kufufuka kwa mungu na Wamisri walioitwa Osiris ili kuwa ikigizwa  kila mwaka kwa miaka kama 2000 kuanzia mwaka 2500 k.m. Brockett,(1979:4) kama ilivyonukuliwa na Mulokozi,M.M.(1996:190).

Huko India, inasemekana drama (tamthiliya) ilitokana na tendi za kidini Mahabhorata na Ramayana, pamoja na miviga iliyofungamana na utendaji wa tendi hizo katika mahekalu ya Kihindu(EA 1982:333; Brockett,1979:240) kama ilivyodondolewa na Mulokozi,M.M. 1996:190). Baadaye drama hizo zilijitenga na udini na kujishughulisha zaidi na masuala ya sanaa na burudani.

Pia huko China, drama ilitokana na sherehe za kidini zilizotendwa na makuhani wa Kibudha kwa kutumia nyimbo, dansa na maigizo bubu.Michezo YA Kichina ni kama vile ya Kijapani, iilkuwa ni faraguzi,hapakuwa na muswada wa mchezo mzima, bali palikuwa na muhtasari tu ambao ulijaziwa na waigizaji wenyewe wakati wa maonyesho. Michezo hiyo ilijitenga na uhalisia, walitumia lafudhi, mavazi na ishara zilizotiwa chumvi makusudi ili kuleta ukengeushi.

Nchini India, palikuwa na drama ya Ki-sangkirt tqngu miaka 200 K.M. Drama hiyo, ilishabihi tendi za kidini za kihindi, daima ilkuwa na lengo la kuleta suluhu au mapatano. Hivyo hapakuwa na tanzia, bali tamthiliya hizo ziliishia kwenye furaha.
Maelezo haya yanatudhihirishia kuwa huenda tamthiliya duniani ilichipuka kutokana na mambo matatu ambayo ni:

i)                   Miviga na viviga vya kijamii na kidini, pamoja na tendi.
ii)                Umathilishaji wa maisha ya kawaida kwa ajili ya burudani, elimu, maonyo au michezo

iii)              Sanaa za maonyesho za kijadi, kwa mfano, ngoma na dansa.   
Ingawa asili ya tamthiliya katika nchi na tamaduni mbalimbali yaelekea kufanana,lakini maendeleo yake yalichukua mikondo tofauti kutegemeana na historia na utamaduni wa jamii inayohusika. Kwa mfano, huko Uyunani(ugiriki),yaelekea tamthiliya za mwanzo zilianza kuandikwa kabla ya mwaka 500K.M. Wayunani walizagawa tamthiliya katika makundi makuu mawili: Tanzia ambao ni drama juu ya mkasa unamsibu mtu mashuhuri kutokana na matukio ambayo mara nyingi hana uwezo nayo, na ambayo yanatokana na udhaifu Fulani alionao na huishia katika majonzi, na komedia ni drama inayokusudiwa kufurahisha, ambayo zaidi iliwahusu watu wa kawaida, na aghalabu humalizikia katika furaha badala ya majonzi. Kwa mfano tamthiliya zilizotungwa na Shakespeare ambazo zilitafsiriwa kwa Kiswahili na Hayati Mwalimu Julius K.Nyerere ni Julias Kaisari (1964), Mabepari wa Venisi (1969).

Kimsingi kuna aina kadhaa za tamthiliya. Kila aina ina sifa zake maalum. Tunaweza kuvitumia vigezo vya muda(duration) na utanzu(genre) kuigawa tamthiliya katika aina mbalimbali.

Kwa mujibu wa kigezo cha muda, kuna tamthiliya ambazo huwa na tendo moja na huchukua muda mfupi. Kwa mfano tamthiliya ya Samuel Beckett iitwayo “Breath” inachukua dakika moja ili hali “maisha ya subira” iliyoandikwa na Omari, S. itachukua muda mrefu kuigiza.

Kigezo cha muda hutegemea wakati ilihali cha utanzu hutegemea yaliyomo(maudhui) au mada ya tamthiliya kutokana na kigezo hiki cha pili tunaweza kuainisha vitanzu vifuatavyo:
          a)     Tanzia (tragegy)
          b)    Futuhi /komedia (comedy)- “usaliti mjini” F. Mbugi
          c)     Melodrama (melodrama) -   “The Begger’s Opera” John Gay, 1728
          d)    Kichekesho (Farce)
          e)     Tanzia- ramsa/ Tanzia- futuhi(tragicomedy)
           f)      Tamthiliya ya kihistoria(Historical play) – Kinjeketile- E. Hussein
          g)     Tamthiliya Tatizo(problem play) – mfano, nguzo mama
              na lina ubani(Penina .M Mhando; Mashetani- E. Husein.
            h)    Tamthiliya ya kibwege (absurd drama)- mfano,                                                            Amezidi(said .A. Mohamed,1995), Upotovu- (Njiru Kimunyi,2000)
       Maelezo hapo juu yanaonyesha kuwa zipo aina nyingi za                                                tamthiliya diniani. Tamthiliya ya Ki- Aristotle ni aina                                                      mojawapo kati ya hizo. Hapa tutaijadili kwa kirefu zaidi                                                   kwa kuwa imeathiri watunzi wengi wa tamthiliya ya Kiswahili.                                         Mulokozi ,M.M.(1996:193), Kwa mujibu wa Ki- Aristotle,                                             tamthiliya yoyote kwa kawaida huwa na vipengele vifuatavyo:-                                        Hadithi(simulio), vitendo, waigizaji wanaomathilisha wahusika wa                                    hadithi, dialogia(mazungumzo). Mazungumzo huweza kuwa ya maneno au ishara.
i)               
                   Hadithi.
   Tamthiliya husimulia hadithi au kisa Fulani. Hadithi hiyo huweza kuwa ya kubuni, au ni   tukio la kweli la historia, au ni mchanganyiko wa yote mawili. Hadithi hiyo kwa               kawaida huhusu mzozo Fulani unaohusisha pande mbili. Upande wa shujaa(mbabe) au    nguli ambaye ni mtendaji mkuu na upande wa mpinzani wa nguli/ mbabe. Hadithi hiyo    husukwa kwa namna inayojenga migogoro wa pande hizo mbili hadi mwisho wake.         Mlokozi,M.M.(1996:193)

   Pia katika jadi ya utunzi wa Ki- Aristotle, mtiririko wa kimatukio kwa kawaida huwa        umbo la piramidi lenye hatua zifuatazo:-

                                                          C
                            B                                                     D

                     A ------------------------------------------------------------ E

Hatua A: Chanzo
      Hapa ndiyo mwanzo/utangulizi wa mchezo katika hatua hii:
-         Hali ya tamthiliya (ya majonzi, ya miujiza, ya nderemo) hudhihirishwa.
-         Mandhari9yaani wakati na mahali panapotokea vitendo vya hadithi) hueleza
-         Baadhi ya wahusika hutambulishwa
-         Taarifa nyingine muhimu (kwa mfano matukio yaliyotangulia kisa hiki) hudokezwa
     Hatua B: Tatizo / kukua kwa mgogoro
           Mvotano kati ya pande mbili au zaidi zinazozozana hujitokeza. Tatizo linalosababisha mgogoro huo hudhihirishwa. Majaribio ya kutanzua mgogoro hufanywa na kushindwa. Kila hatua muhimu katika ukuaji wa mgogoro huo huitwa kipeo(turning point), vipeo kadhaa vidogo huweza kufikiwa kukiukwa bila usuluhishi.\

Hatua C: Kilele
Mantiki ya mvutano na matukio hatimaye hufikisha hadithi kwenye kilele(climax) katika hatua hii mzozo hufikia kiwango cha juu kabisa pasi na uwezekano wa kurudi nyuma.
       
Hatua D: Mshuko
Katika hatua hii mvotano huanza kulegea na hutokea mshuko wa taharuki. Mgogoro huwaelekeza wahusika kwenye pambano la mwisho la mkataa.
     
  Hatua E: Mkasa/ suluhisho
Katika kipengele hiki, kama tamthiliya niya kitanzia, mbabe/nguli hushindwa ama kupatwa na mauti ama maanguko, na mgogoro hufikia hatima yake. Na kama tamthiliya ni komedia, mvotano baina ya pande zinazozozana husuluhishwa na hali ya utangamano hurejeshwa.
    
 ii) Vitendo
Tamthiliya nyingi za Ki- Aristotle hugawanyika katika sehemu ziitwazo vitendo(act) kila kitendo huzingatia tendo moja kuu ndani ya mchezo. Kwa mfano:- katika mpangilio wa matukio hapo juu, kila kipengele kingeweza kuwa kitendo kimoja. Hivyo tamthiliya yenye mpangilio huo kijadi iltakiwa kuwa na vitendo vitano.

Onyesho(scene)
Kila kitendo hugawanyika katika sehemu ndogo ziitwazo maonyesho. Onyesho (scene)moja kwa kawaida huwasilishwa tukio moja linalotendeka mahali pamoja. Kwa kawaida onyesho moja hutenganishwa na jingine kwa kuzingatia mantiki ya kile kinachosimuliwa, tukio moja likimalizika onyesho nalo huwa limemalizika. Wakati wa maigizo jukwaani mabadiliko ya maonyesho huashiria kwa kufunga pazia au kuzima taa, au kwa wahusika kuondoka jukwaani.

   iii) wahusika na waigizaji
Usawili wa wahusika wa tamthiliya hufanywa kwa njia ya matendo, kwani fursa ya kutoa maelezo marefu haipo. Wahusika wa tamthiliya hawana tofauti na wahusika wa hadithi, huweza kuwa mviringo, bapa, watu wa tabaka la juu, wanyonge, n.k. Pia huwa na wahusika wakuu na wadogo.

Wahusika wakuu
Nguli /mbabe: Shujaa wa tamthiliya ambaye matendo mengi yanahusu maisha na majaliwa yake, kwa mfano, Kinjeketile katika tamthiliya ya Kinjeketile –Hussein,E. (1969), Ndiye nguli /mbabe (hero) yaani mhusika kiini alikuwa ni mtu wa tabaka la juu ambaye aliangamia kutokana na ama ila fulani katika tabia au maamuzi yake –( tragic flow) kwa sababu ya kusukumwa na mazingira yanayomzidi uwezo.

Wahusika wadogo
Hawa anghalabu huwa ni wengi, baadhi yao huwa na jukumu dogo tu katika tamthiliya na hutokea mara chache.

Waigizaji
Mara nyingine huitwa wamathali. Hutokea jukwaani mahali pa wahusika wa mchezo na kuiga vitendo na tabia za hao wahusika wanaowawakilisha.

iv)              Dialogia (mazungumzo ya wahusika)
Tamthiliya husonga mbele kwa njia ya vitendo na mazungumzo ya wahusika. Baadhi ya tamthiliya huwa na monolojia, mhusika huzungumza mwenyewe kudhihirisha mawazo aliyonayo moyoni. Zipo tamthiliya zinazotumia masimulizi, ambapo hutokea msimulizi na kueleza mambo yaliyotokea, mithili ya mtambaji wa hadithi au utendi. Mbinu hii hutumika katika drama- tendi. Baadhi ya tamthiliya za Kiswahili zimefuata mbinu hiyo ya Ki- Aristotle kwa mfano: Mulokozi,M. Mukava wa Uhehe, (1979).


Historia ya Tamthiliya ya Tanzania.
Kabla ya kuja kwa Ukoloni tamthiliya haikuwepo nchini. Aina za sanaa za maonyesho zilizokuwepo zilitofautiana na tamthiliya hii iliyoingizwa na tamaduni ngeni. Chuo kikuu huria cha Tanzania (1997:39).
Bertoncini,1989, kama ilivyodondolewa na Wafula,Richard,(1999:3) anafafanua kuwa: Tamthiliya kama utanzu wa fasihi- andishi katika lugha ya Kiswahili imeanza kushughulikiwa juzu juzi, mchezo wa kuigiza ulioandikwa ulikuja na wakoloni. Mgeni aliyejihusisha na uigizaji hapo mwanzomwanzo aliitwa Graham Hyslop mnamo mwaka 1936 alitunga filamu iliyoitwa, “Akili ni mali” Tamthiliya ilianza Tanzania wakati wa Ukoloni miaka ya 1920, tamthiliya hizo zilizo nyingi zilikuwa za kidini.

Tamthiliya zilizoandikwa ili zigezwe jukwaani hazikuwepo kabla ya Ukoloni. Badala yake, zilikuwepo tamthiliya zisizoandikwa, ziligezwa au kufaraguzwa kwa ajili ya kuonyeshwa kwenye shughuli maalum, kwa mfano, kwenye sherehe za jando na unyago, mazishi, kutawazwa kuwa mtemi, arusi na michezo ya watoto. Tamthiliya hizo zilikuwa na sifa kadhaa za kitamthiliya, yaani hadithi, vitendo, wahusika, na waigizajiwao na dialogia. Kadhalika zilkuwepo na sifa saba za sanaa za maonyesho, nazo ni:

 i) Dhana inayotendeka          v) hadhira
ii) Uwanja unaotendewa         vi) kusudio la kisanii
iii) Watendaji                           vii) muktadha wa kisanaa
iv) Ubunifu (umathilishaji)

Muhando Mlama na Balisidya 1976:4 na Mlokozi, M . M.(1996:189).
Tamthiliya hizo hazikuwa na ploti ya Ki- Aristotle wala matini yaliyoandikwa. Hivyo zilikuwa ni tamthiliya – simulizi. Mulokozi, M.M.(1996:203).
Anaendelea kudondoa kwa kutolea mfano michezo ya watoto katika kuigiza , umama, mtoto wa kike au wakiume n.k.  Mchezo huu ni tamthiliya halisi yenye kumathilisha maisha.


Tamthiliya andishi ya Kiswahili
Tamthiliya za Kiswahili zilizoandikwa kwanza kabla ya kuigizwa jukwaanizilianza kutokea miaka ya 1950.  Tamthiliya za mwanzo zilikuwa za kidini. Kwa mfano, ilichapishwa tamthiliya ya Frank, C.(1951) iliyoitwa “Imekwisha” (Mulokozi,M.M. 1992:205).

Tamthiliya za mwanzo zisizokuwa za kidini zilianza kutungwa kati ya 1952 na 1956. Shughuli za tamthiliya wakati huo zilisimamiwa na Graham Hyslop, Mwingereza aliyekuwa katika utumishi wa serikali ya kikoloni ya Kenya. Pia alianzisha kikundi cha maigizo kwa ajili ya askari mwaka 1944, na miaka ya 1950 alianza kutunga michezo ambayo iliigizwa na kikundi chake. Michezo ya mwanzo katika lugha ya Kiswahili ni “Afadhali Mchawi” (1957), na “Mgeni Karibu” (1957), hata hivyo Hyslop alianza kuzunguka katika shule na vyuo mbalimbali nchini Kenya akifundisha muziki na uigizaji.
Miongoni mwa wanafunzi wa mwanzo wa Hyslop waliokuwa wakisoma “Alliance high school” ni Henry Kuria, Kimani Nyake, Gerishon Ngugi na B.M.Kurutu. Tamthiliya ya Kuria, ‘Nakupenda Lakini’ (1954) iliigizwa kwa mara ya kwanza 1957, ya Nyake , ‘Maisha ni Nini’ iliigizwa mwaka 1955, ya Gerishon Ngugi, ‘Nimelogwa nisiwe na Mpenzi’(1961) iliigizwa mwaka 1956, na ya  Kurutu ‘Anatakiwa Polisi’ mwaka 1957, kwa mujibu wa Ngugi wa Thiong’o(1981:39) kama ilivyodondolewa na Mulokozi,M.M. (1996:205).

Kwa ujumla tulipopata uhuru, tamthiliya zote za Kiswahili zilizochapishwa zilikuwa zimeandikwa na Wakenya. Watanzania hawakujitokeza katika uwanja huu hadi baada ya uhuru. Kwa mujibu wa Mulokozi,M.M.(1996:205).

TAMTHILYA WAKATI WA UHURU
Tamthilya ya kizungu iliendelea kuigizwa hata baada ya uhuru, mashuleni na katika kumbi maalum za maonyesho kama ‘Little Theatres’. Hata hivyo, umaarufu wake ulipungua kiasi, hususan kwa upande wa Tanzania. Mulokozi, M.M.(1996:207)
Anaendelea kufafanua, licha ya tamthiliya za kizungu, hali kadhalika tamthiliya za kiafrika zilianza kuandikwa kwa lugha za Kigeni na zingine za kiafrika, zilifasiriwa kwa Kiswahili, kwa mfano, “I will marry when I want” (1982) ilifasiriwa kwa Kiswahili, “Nitaolewa nikipenda” (1982) na Ngugi wa Thiong’o na Ngugi wa Mirii.

Watanzania waliathiriwa sana katika masuala ya sanaa za maonyesho za kigeni kiasi kwamba waliweza kujishirikisha kikamilifu katika kutunga tamthiliya na kuzionyosha majukwaani. Tamthilya hizi hazikuwa na maana yenye uzito wowote kwa tamaduni zao.  Tamthiliya hizo ziliongelea juu ya jamii ambayo watanzania hawakuifahamu wala kuielewa wao walivutiwa na mavazi ya washiriki, matumizi ya taa za rangi na kadhalika, 

Mlama, P.(1987:119) vol.54/2 jarida la Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili .
Mlama , P.(1987:119- 120) anasisitiza, kutokana na tamthiliya za kimagharibi kutokidhi mahitaji ya watanzania ndipo ilipowapelekea wasanii hao kuanzisha vichekesho.
Mlama, P.M.katika makala ya semina ya kimataifa ya uandishi wa Kiswahili iii,(1983:206- 207), afafanua kuwa drama ililetwa Tanzania na Waingereza. Drama iliigizwa mashuleni ambapo wengi wa walimu walikuwa Waingereza. Madhumuni ya kuigiza drama haikuwa na uzito mkubwa.  Hasa Waingereza walikuwa na kitu cha kupitisha muda, wakati ambapo walikuwa hawna la kufanya. Waliona kuendesha drama kwao ni jambo borakwani ilihusu utamaduni wa kwao na kuweza kujikumbusha kwao. Kwa mfano tamthiliya za William Shakespeare, Julius Ceasar, Macbeth, n.k. hazikuwa na maana muhimu kwa watanzania kwani walioshiriki walikuwa wanakariri tu maneno bila kuelewa yale waliyoyasema, mara nyingi tamthiliya hizi zilikuwa na lengo la kuburudisha tu.

Mlama , naendelea wakati drama hii ya kigeni ilpoendelea kushika mizizi chini ya udhamini wa wazungu. Iliibuka aina nyingine ya drama, hii ni ile ijulikanayo kama, “vichekesho”hii ilitokea kwasababu watanzania ambao walivutiwa kutumia vipaji vyao vya kisanaa kuonyesha tamthiliya, lakini hawakuwa na ujuzi wa ndani wala iwezo wa utunzi na uonyeshaji wa tamthiliya kiasi cha kutoa kazi sawa na zile za wataalam wa 

Kiingereza. Badala yake walianzisha kitu kinachofanana na tamthiliya lakini ambacho waliweza kutunga na kuonyesha kutokana na uwezo wao wenyewe. Juhudi zao zilitoa aina ya drama iliyojulikana kama “vichekesho”.

Hii haina maana kuwa vichekesho vilikuwa duni kuliko drama ya wageni.  Bali vichekesho vilitoa drama iliyokuwa na tabia kisanaa tofauti na drama yenyewe. Kwa mfano, vichekesho havikutegemea tamthiliya ilyoandikwa bali, tungo zake zilitungwa palepale wakati wa kutenda, vichekesho vilihusu maisha ya kawaida ya Tanzania ya wakati ule, wakati ile drama nyingine ilihusu jamii za Ulaya. Mfano wa kichekesho cha wakati huo ni “Mshamba wa Kioo”

Baada ya uhuru vichekesho vilichukua sura tofauti kidogo. Badala ya kuwasuta “washamba” vilianza kuwasuta “wazungu weusi” Waafrika wanaoringia elimu au vyeo vyao na kudharau utamaduni wao. Kwa mfano, G. Uhinga, 1968, pia viliongelea masuala mbalimbali kwa mfano , matatizo ya kifamilia, ukosefu wa kazi, ukimwi,  uhalifu na udanganyifu waganga wa jadi n.k.M.M.Mulokozi(1996:206)
Naye Lihamba,(1985:281) kama alivyodondolewa na M.M. Mlokozi(1996:206) anasisitiza; vipo vichekesho vya kisiasa vyenye kuzungumzia siasa ujamaa, ubinafsi wa uongozi, matatizo ya kuanzisha vijiji vipya n.k. Anaendelea kusisitiza,
“Beside their informality and flexibility, these plays have two major Other characteristics: they have displayed a strong alignment with the political and social issues after Arusha and have a strong comedic bias.  The tendency to favour comedic elements or play for laugh has endowed.  The plays with the collective name of vichekesho.  This has been irrespective of the nature of the content and the performance objectives.”

Tafsiri:
Hata hivyo baadhi ya vichekesho vya Radio Tanzania, kwa mfano,  “mahoka” kipindi kilichoanza mwaka 1974 na “pwagu na pwaguzi” mwaka 1979 hukejeli na kukemea tabia mbovu za baadhi ya watu, wakiwemo viongozi wa kisiasa. Tasnifu ya Lihamba(1985) imeonyesha kuwa baada ya Azimio la Arusha nchini Tanzania vikundi vya ngoma na maigizo kama ishirini na nane(28) mara kwa mara vilionyesha maigizo yaliyohusu siasa. 

Baadhi ya maigizo hayo yalitukuza siasa ya ujamaa na kutangaza kampeni mbalimbali za wanasiasa. Lihamba, (1985:498- 502). Hata hivyo kwa sasa vichekesho hutangazwa katika vituo vya redio na televisheni, na huonyeshwa kwenye kumbi za starehe.

Baada ya uhuru, utunzi wa tamthiliya ulipamba moto zaidi, hasa upande wa Tanzania. Mashindano ya utunzi na uigizaji yaliendeshwa na Youth Drama Association nchini Tanzania yaliwawezesha watunzi chipukizi kujitokeza, akiwemo Ebrahim Hussein ambaye tamthiliya yake ya kwanza , “wakati ukuta” 1969 ilishinda tuzo katika mashindano hayo. Wakati huo huo ndipo walipojitokeza watunzi waliohitimu chuo kikuu cha Dar es Salaam. Baadhi yao ni Ebrahim Hussein mwenyewe, Penina Mhando(Mlama), N.Ngahyoma na G. Uhinga.

Miaka ya 1970- 1974 ilishuhudia kuchapishwa kwa tamthiliya nyingi za Kiswahili. E.Hussein alichapisha, Kinjeketile(1969), Mashetani(1971), Jogoo Kijijini na Ngao ya Jadi(1976), Arusi(1980) na Ukingo wa Thim(1989).
Penina Mhando, alichapisha “Hatia”(1972), Tambueni Haki Zetu(1973), Pambo(1975), Nguzo mama(1982), Lina Ubani(1984); Pia watunzi wengine waliojitokeza kipindi hiki ni Emmanuel Mbogo, “Giza Limeingia”(1980), Tone la mwisho,(1981), Ngoma ya Ngwanamalundi(1988), Morani, (1993); watunzi wengine ni M. M. Mlokozi, S.A. Mohamed, E. Semsaba na E. Kezilahabi.

Orodha hii ya watunzi inatosha kueleza kuwa utunzi wa tamthiliya ya Kiswahili umepiga hatua kubwa tangu mwaka 1970. Kimaudhui tamthiliya hizo zilianza kusawiri mazingira ya waswahili kwani kwa kuchunguza suala la maudhui tunaweza kuzigawa tamthiliya za Kiswahili za miaka ya 1960- 1994 katika migogoro kama ifutavyo:
Kuna migogoro ya kitamaduni: Dhamira hii inajitokeza katika umbo la mgongano wa  utamaduni wa kijadi na kiafrika na utamaduni wa kizungu au kati ya mjini na shamba, dhamira hii imejadiliwa zaidi katika baadhi ya kazi za E,Hussein, wakati ukuta na kwenye ukingo wa thim.

Pia matatizo ya kijamii kwa mfano, mapenzi, ndoa, ufukara, urithi, n.k, vimejadiliwa zaidi katika tamthiliya ya, Nakupenda Lakini  na Nimelogwa nisiwe na Mpenzi.
Si hizi tu bali wasanii wa tamthiliya wa kipindi hiki waliangalia jamii jinsi inavyoishi na kuweza kutunga kazi zao kusawiri mazingira husika. Kwa mfano maudhui katika tamthiliya yalikuwa pia; ukombozi na utaifa, ujenzi wa jamii mpya, mfano tamthiliya ya E. Mbogo, Giza Limeingia, na E. Hussein, Mashetani. Mwanamke na matatizo ya kijinsia mfano Nguzo Mama(Mhando), Machozi ya Mwanamke(Ngozi), na falsafa ya maisha mfano E.Kezilahabi.

Katika kazi hii si lengo la mwandishi kueleza historia ya tamthiliya pekee bali sasa tulejee katika swali la msingi ambalo ni mgogoro katika tamthiliya ya Kiswahili. Tamthiliya yakiswahili hasa zile zilizoandikwa, baadhi yake zximejaa mbinu za Kimagharibi. Nyingi zina muundo wa Ki- Aristotle, zinatumia dialogia, zina vitendo, maonyesho na migogoro inayosuluhishwa mwishoni; M.M. Mlokozi,(1996:197).
Aristotle ni mwanafalsafa wa Kiyunani aliyeishi Uyunani(Ugriki ya kale) kati ya mwaka 386 na 322 kabla ya kristo. Baada ya maandishi yake, maandishi ambayo yamekuwa na athari kubwa katika maendeleo ya taaluma za Ulaya kwa karne nyingi ni kitabu chake juu ya, “sanaa ya utunzi” alichokiita “Poetics’ambamo anafafanua sheria au kanuni za utunzi wa tamthiliya,ambazo kwa muda mrefu sana zilichukuliwa na wanasanaa wengi wa michezo ya kuigiza kama mwongozo karibu kote Ulaya. Ebrahim Hussein kama alivyodondolewa na makala za semina ya kimataifa ya maandishi ya Kiswahili,(1983;197).

Anaendelea kusisitiza, Myunani huyu anatambua vipengele sita; sehemu ya nyimbo, matamshi, mtiririko wa vitendo, wahusika, fikra na utumiaji wa jukwaa. Pia anaona umuhimu kuwa mchezo huu ni wa kufurahisha na kuchekesha au ni wa kuhuzunisha na kuleta majonzi.

Vile vile baada ya kutambua vipengele sita hivyo, Aristotle anaugawanya mchezo wa Kiyunani katika sehemu tatu, sehemu ya kwanza ni ile ya mwanzo au utangulizi, sehemu ya pili ni kitendo chenyewe. Anapendelea wimbo uimbwe katika sehemu ya mwisho. Lakini waandishi wengi wa michezo ya kuigiza karne na karne hawakufuata mapendekezo haya. Kwa mfano Shakespeare katika mchezo wake wa “Mfalme Lear” anamfanya kichaa aimbe mara nyingi. Pia Ngugi wa Thiong’o katika mchezo wake wa, “Dedan Kimathi” anatumia nyimbo hata mwanzoni mwa mchezo.

Aristitle alipendelea kuwa mwandishi mchezo wa kuigiza ayafahamu mambo haya ni kuandika matamshi katika umbo lenye mizani.Said A.Mohamed (1995;59).
Anaendelea kufafanua, lakini si waandishi wengi wa tamthiliya wanatumia lugha ya kishairi na yenye mizani katika michezo yao. Kwa mfano; Soyinka katika mchezo wake wa  “wale wanaoishi kwenye mabwawa” yeye hatumii ushairi; au Penina Muhando katika mchezo wa “Pambo” yeye pia hatumii lugha ya kishairi na yenye mizani. Na Zola yeye anapinga kabisa utumizi wa lugha ya kishairi katika mchezo wa kuigiza. Zola anaungwa mkono katika hili na waandishi wengi kwa mfano Ibsen na wengine. Wao wanaunga mkono utumiaji wa mazungumzo ya kitamthiliya (yaani- dramatic dialogue).
Ebrahim Hussein katika makala za semina ya kimataifa ya waandishi wa Kiswahili, 1983:202- 203 anafafanua; Wasanii wengi hawakubaliani nayo nadharia ya Aristotle inayosisitiza mpangilio huo wa mtiririko wa vitendo,hasa vile kuwa unasisitiza kilele na unasiositiza kwamba kitendo kinachopaswa kuigizwa ni kile chenye kutia hofu na huruma moyoni.

Brecht, anaona kwamba Aristotle amempa mwandishi au mwigizaji wa tamthiliya nafasi nyembamba. Mila nyingi za uigizaji, kwa mfano mila za kiafrika , kijapani na kihindi hazikubaliani na hizo njia nyembamba. Lewis Nkosi anasema, dhahiri uandishi namna hii yaani unaofuata misingi ya Aristotle, haswa huu wa mpangilio wa mtiririko na vitendo unakwenda dhidi ya mila za kishairi katika Afrika.

Hivyo basi, kuandika tamthiliya kwa kufuata misingi ya Ki-Aristotle ni njia moja ya kuandika tamthiliya, lakini hiisi njia pekee. Na kweli mila ya kiafrika haiowani vizuri na usanifu huu. Pengine njia isiyokuwa ya Aristotle ni muafaka zaidi, hata hivyo ikiwa mwandishi atatumia misingi ya Aristotle au baadhi ya misingi hiyo, jambo muhimu ni kuweka akilini kwamba misingi hii si sheria ila ni vipengele vya tamthiliya. Sheria Kama ipo ni moja tu, kujua nini watu wanapenda kuona na kusikia jukwaani kwa kuangalia ujumi wa wakati husika. Ni vizuri mwandishi wa mchezo wa kuigiza kuwanayo sheria hii kichwani wakati anapoandika mchezo wa kuigiza. Maelezo hayo hapo juu yanaungwa mkono na P. Mlama, alivyodondolewa na makala za semina ya kimataifa ya waandishi wa Kiswahili, 1983:216.

Tutazame kwa kifupi ni vipengele gani muhimu katika utunzi wa tamthiliya. Lakini ieleweke wazi kuwa nia si kutoa fomula inayofaa kutumiwa katika utunzi wa tamthiliya, utunzi wa sanaa hauwezi kuwekewa fomula kwasababu msanii anapotoa kazi ya sanaa anunda kitu kipya na kutokana na kipaji chake cha kisanii wakati anaunda kitu hiki anaweza anaweza kuunda mbinu mpya pale ambapo zile zinazojulikana hazimwezeshi kukamilisha kile anachokiunda. Misukumo inayotokana na mabadiliko mbalimbali katika jamii ya wakati wake humlazimisha msanii kutumia mbinu mpya tofauti na zawaliotangulia. Na kwamba msanii anayeridhika na mbinu zilizopo anadhihirisha upungufu wa uwezo wake wa kisanii.

Pia M.M.Mlokozi, (1996:210- 211) anafafanua kuwa watunzi wachache kuanzia miaka ya 1970, hawakuridhika na upokeaji wa mbinu na kanuni za tamthiliya ya ulaya, hasa ya Ki-A ristotle, walihisi kuwa palihitajika tamthiliya ya kiafrika yenye kuchota mbinu zake kutokana na sanaa za jadi za kiafrika. Hivyo watunzi hao walianzisha maigizo ya kimajaribio.
Miongoni wanamajaribio hao wa mwanzo ni Ebrahim Hussein. Mtunzi huyu alijaribu kutumia mbinu za utambaji wa ngano katika maigizo yake ya Ngao ya jadi na Jogoo kijijini.

Penina Mhando pia, katika tamthiliya zake za “Lina Ubani, na Nguzo Mama”pia alijaribu kutumia mbinu ya utambaji wa ngano.
P .O. Mlama, kama alivyonukuliwa na makala za semina ya kimataifa ya waandishi wa Kiswahili,(1983:215) ansisitiza; Baadaye utanzania uliweza kuonekana zaidi katika fani wakati watunzi walipojaribu kutumia vipengele Fulani Fulani vya fani za sanaa za maonyesho zenye asili ya Tanzania katika kuandika tamthiliya hizo. Majaribio haya ni kama ya kutumia nyimbo, utambaji hadithi, majigambo katika utunzi wa tamthiliya kwa mfano katika ‘Tiba’, (Nkwera,1969), Pambo(Mhando,1975), Harakati za Ukombozi (Lihamba na Balisidya, Matteru,1978), Kinjeketile(Hussein, 1969) n.k. Majaribio hayo yameleta upya katika fani ya tamthiliya ambayo iltegemea zaidi usanii wa vitendo na usemaji tu.

Kwa kuhitimisha kazi hii mwandishi anasema majaribio ya kufanya tamthiliya ioane na utamaduni na mazingira ya kiafrika bado yanaendelea, na ni vigumu  kwa wakati huu kubashiri hatima yake itakuwaje. Yamkini kutokana na majaribio kama haya tutapataaina ya tamthiliya tunayoweza kuiita ya kiafrika au ya Kiswahili.    

Hakuna maoni: