Jumatano, 15 Julai 2015

Kategoria za kisarufi na Maana ya sintaksia



Kategoria za kisarufi
Kategoria ya kisarufi ni kundi la maneno lenye sifa za kisarufi zinazofanana.
Kwa mfano, mtoto, embe, kiti, mti n.k. ni maneno ya kategoria
nomino kwa sababu yana sifa shirika. Maneno ya kategoria moja ya kisarufi yana sifa za kisemantiki, kimofolojia au kisintaksia zinazofananana ambazo ziwapo katika tungo hujaza nafasi karibu ileile.
Nomino – hutaja jina la kitu, huwa mtenda au mtendwa katika sentensi,
huweza kuwa katika umoja au wingi. Kwa mfano: mtoto – watoto, kitu – vitu, embe –maembe.
Kitenzi – huonyesha tendo au hali ya kufanyika kwa kitu. Kwa mfano: cheza, imba, kimbia.
Kivumishi – hueleza sifa ya kitajwa ambacho ni nomino. Kwa mfano: dogo, zuri
Aina nyingine za maneno ni pamoja na kielezi, kiunganishi, kihusishi n.k.
Aina za maneno hutumika kubainisha aina za virai kwani jina la kirai hutokana na kategoria ya kisarufi ya neno kuu.

Maana ya sintaksia
Sintaksia ni tawi la isimu ambalo linahusu namna maneno yanavyoungana na kuhusiana katika kirai au sentensi. Sintaksia inachunguza namna maneno yanavyojipanga katika sentensi kwa kuzingatia kanuni za sarufi ya lugha husika.

Mikabala tofauti ya Sintaksia
Uchambuzi wa muundo wa lugha umefanywa na wanasarufi wa nyakati tofauti na kuzua mikabala tofauti kuhusu muundo wa lugha kama walivyouona kwa wakati wao. Mkabala wa awali uliokuwa umejikita katika lugha kongwe kama Kilatini ulikuja kujulikana baadaye kama wa kimapokeo kwani ndio uliorithishwa kutoka kizazi hadi kizazi na kutumika kuchambua
lugha nyingine za dunia. Mkabala mwingine ni ule ulioichambua lugha kwa kuzingatia vijenzi vinavyounda sentensi na ulioasisiwa na Chomsky. Mkabala huu ulijulikana kama mkabala wa kimuundo ambao hata hivyo baadaye ulifanyiwa marekebisho zaidi na mwenyewe Chomsky na waliomfuata.

Mkabala wa Kimapokeo
Wanamapokeo walichambua sintaksia ya lugha kwa kuainisha miundo ya sintaksia iliyo katika lugha. Kwa mujibu wa wanamapokeo, virai na sentensi zimeundwa na kategoria za kisarufi yaani maneno ambayo kila moja liliainishwa na uamilifu wake kutajwa. Kwa hivyo mwanaisimu alichambua sentensi kwa:
a) kutaja kategoria za kisarufi za maneno yanayounda sentensi
b) kueleza kazi au uamilifu wa kila neno lililounda sentensi.

Kwa mfano: ‘Mama anapika chakula’.
Sentensi hii ilichambuliwa kwa kueleza:
Muundo: Sentensi hii inaundwa na maneno matatu: ‘mama’, ‘anapika’ na ‘chakula’ na kwamba kila neno lina kategoria yake
Kategoria za maneno yanayounda sentensi: ‘mama’ na chakula’ ni nomino za umoja, na ‘anapika’ ni kitenzi kilicho katika wakati uliopo.
Uamilifu wa kila neno: ‘Mama’ ni kiima, ‘anapika chakula’ ni kiarifu.
Aina ya sentensi: Sentensi hii ni kishazi. Hii ni sentensi arifu.
Aidha wanamapokeo walichambua sentensi kwa kubainisha kategoria za maneno yaani aina za maneno kwa mujibu wa maana zake, vipengele vya kimofolojia na au tendo.
Nomino ilifafanuliwa kuwa ni jina la kitu, mtu, mnyama, hali. Nomino huweza kuhesabika au kutohesabika na kwamba huwa na umoja na wingi au umoja tu au wingi tu.
Kitenzi kilifasiliwa kuwa ni neno lenye kudokeza tendo ambalo huchukua viambishi vya wakati uliopo, uliopita au ujao, mtenda ambaye huwakilisha kiima katika kitenzi , mtendwa n.k. Katika sentensi kitenzi hufuata kiima ambacho ni nomino mtenda au kufuatwa na nomino mtendwa au yambwa. Kwa hivyo sentensi ‘ Mama amelala’ ingechambuliwa hivi:
Sentensi hii ina nomino ‘mama’ ambayo ina uamilifu wa kiima cha sentensi yaani mtenda na kitenzi ‘amelala’ chenye uamilifu wa kiarifu cha sentensi. Kitenzi hiki ni sielekezi.

Mkabala wa wanamiundo kama ulivyoasisiwa na Noam Chomsky
Nadharia ya Sintaksia ambayo mwasisi wake ni Noam Chomsky imejaribu kueleza vipengele vya kisintaksia vya lugha mbalimbali ili kuonyesha jinsi lugha mahsusi zinavyopanga maneno yao ili kupata sentensi

Lengo la Chomsky katika uchanganuzi wake wa lugha ni kuunda nadharia ya sintaksia ya jumla itakayonyesha vipengele vya kisintaksia vinavyopatikana katika kila lugha na jinsi vinavyotofautiana. Hii inafahamika kama nadharia ya sarufi ya jumla.
Lengo lingine la Chomsky ni kupinga mtazamo wa wanaisimu wa miaka 1950 (wanamapokeo) waliodai kuwa tofauti za lugha hazina ukomo, mtazamo ambao hakuuafiki kwani ulimaanisha kuwa ingebidi kila lugha iwe na nadharia yake. Alidai kuwa tofauti baina ya lugha ni ndogo na kwamba nadharia ya sarufi ya lugha ingeweza kujumuisha lugha zote isipokuwa kwa tofauti ndogondogo tu. Alibainisha kategoria za virai kuwa ni: KN, KT, KV, KE, KH, KU.



Sarufi miundo virai
Muundo ni mpangilio wa vitu vidogo vilivyowekwa pamoja na kujenga kitu
kikubwa zaidi.
Sarufi miundo virai ni mkabala wa kuchambua lugha kwa kuigawa sentensi katika virai vinayoiunda na kisha kuvichanganua zaidi hadi kufikia neno moja moja lililokiunda kirai.
Tungo huundwa na viambajengo kwa utaratibu maalumu.Tungo za lugha ni neno, kirai, kishazi na sentensi. Virai, vishazi na sentensi huundwa na maneno.

Muundo wa kirai na sentensi
Kirai, kishazi na sentensi ni vipashio vya lugha vinavyoundwa na viambajengo ambavyo ni vidogo kuliko vyenyewe. Kirai hujengwa na maneno, na kishazi na sentensi hujengwa na virai. Viambajengo vya tungo ndivyo vinavyofanya muundo wa tungo husika.

Muundo wa Kirai
Kirai ni fungu la maneno yanayohusiana kimuundo lisilokuwa na muundo wa kiima kiarifu. Maneno katika kirai humilikiwa na neno moja ambalo ndilo neno kuu. Kirai hubainishwa na kategoria ya neno kuu. Kwa mfano: KN, KT, KV, KE KH n.k.
Virai huundwa na viambajengo. Kiambajengo ni kikundi cha maneno au hata neno moja pia inayofanya kazi kama kitu kimoja. Kirai, kishazi au sentensi ni mkusanyiko wa viambajengo kadha.
Kirai ni mkusanyiko wa viambajengo vilivyojengwa kuzunguka neno kuu. Kwa mfano, KN huundwa na nomino na vivumishi vyake, kwa hivyo muundo wa kirai ni maneno yanayokiunda yakiwakilishwa na alama za kategoria za maneno hayo.
Kwa mfano: 

a) ‘Mtoto mdogo’.
Hiki ni Kirai Nomino (KN) kilichoundwa na N (nomino) na V (kivumishi).
Kwa hivyo KN à N+V
b) ‘analima shamba’.
Hiki ni kirai kitenzi (KT) chenye kuundwa na kitenzi (T) na kirai nomino (KN). Kwa hivyoK
T à T+KN
Muundo wa Vishazi na Sentensi
Kishazi ni kikundi cha maneno kilicho ndani ya sentensi chenye muundo wa
kiima na kiarifu. Kishazi kina muundo sawa na sentensi.  
Aina za vishazi na miundo yake
a) Vishazi ambatani
b) Vishazi tegemezi
Sentensi na Miundo yake
Sentensi ni kikundi cha maneno chenye maana iliyo kamili. Sentensi ndicho kipashio lugha cha kimuundo ambacho ni kikubwa kuliko vipashio vingine. Vipashio vya lugha ni pamoja na: mofimu, neno, kirai, kishazi na sentensi yenyewe. Sentensi na kishazi huundwa na virai vikuu viwili: KN na KT. KT yaweza kuundwa na kitenzi na nomino, kitenzi na kielezi n.k.
Kwa hivyo S-à KN + KT
Sentensi na upatanishi wa kisarufi

Sarufi geuza umbo zalishi
Nadharia geuza umbo zalishi huonyesha ujuzi alionao mzungumzaji ambao humwezesha kutunga sentensi sahihi na zisizo na kikomo. Uwezo wa mzungumzaji kutunga sentensi zisizo na ukomo unatokana na kufahamu kanuni za kutunga sentensi sahihi ambazo mzawa wa lugha anazijua kutokana na kuwa na umilisi na lugha yake. Kanuni za kutunga sentensi sahihi hubainisha sentensi sahihi na zisizo sahihi.
Kwa mujibu wa nadharia hii, sentensi ina umbo la nje ambalo ndilo linalojitokeza katika usemaji na hata inapoandikwa, na umbo la ndani ambalo huwa limefichika na hujidhihirisha katika umbo jingine wakati wa kuongea (maana).