Alhamisi, 28 Julai 2016

DONDOO KUHUSU UHUSIANO BAINA YA LUGHA NA JAMII

DONDOO KUHUSU UHUSIANO BAINA YA LUGHA NA JAMII@
Okoa Simile



       a   .      Lugha ni nini?
Lugha - ni mfumo wa sauti za nasibu zilizokubaliwa na watu au jamii ili zitumike katika mawasiliano yao ya kilasiku ili kueleza hisia, mawazo, matakwa na mahitaji yao.


      b       .      Jamii ni nini?
Jamii - ni kundi la watu wanaoishi katika eneo Fulani, wanao jitambulisha kama kundi moja, wenye utamaduni mmojana na  lugha moja.

      c     .       Isimu jamii ni nini?
Isimu Jamii - ni tawi la isimu (elimu ya lugha) linalochunguza namna lugha inavyotumika katika jamii na uhusiano baina yake. Tawi hili huzingatia matumizi ya lugha katika mazingira tofauti; aina mbali mbali za lugha na mazingira yake; uhusiano kati ya lugha na utamaduni wa jamii inayoitumia.
King’ei (2010), anaeleza kuwa, kwanza lugha ni zao la jamii, na ni kipengele muhimu sana cha utamaduni wa jamii husika. Pili, lugha hutumiwa na jamii kuhifadhi amali na utamaduni wake na hasa kama chombo maalumu cha kuwezesha wanajamii kuwasiliana. Hivyo isimu jamii hueleza na kufafanua mahusiano ya karibu kati ya lugha na jamii ambayo ndiyo mama wa lugha
.
       d      .      Uhusiano huu baina ya lugha na jamii.
               i.            Lugha ni zao la jamii, ni sehemu ya jamii kwani ni sehemu ya utamaduni wa jamii husika. Lugha ni njia inayotumiwa na wanajamii ili kueleza na kusambaza utamaduni wake.
         ii.            Mwanaisimu Sapir na Whorf, wanaeleza kuwa lugha huathiri sana na kudhibiti jinsi wazungumzaji na watumiaji wa lugha wa jamii fulani wanavyoufasili ulimwengu wao. Kulingana na wanaisimu hawa muundo wa maana katika lugha ndiyo msingi wa mawazo au utaratibu wa fikra. Mwanadamu hawezi kufikiri kamwe bila kutumia lugha. Jambo hili linamaanisha kuwa kwa vile mawazo na fikra za mwanadamu vinaukiliwa na lugha  basi inawezekana kudhibiti fikra za wanajamii kwa kuidhibiti lugha yao. Katika muktadha ya Kitanzania nan chi nyingi za Kiafrika , hili limthibitika kwani, miongoni mwa Watanzania walio wengi wanahusisha maarifa na lugha fulani (mathalani kiingereza). Hii inatokana na imani iliyopandikizwa na wakoloni kwamba lugha ya Kiingereza ni lugha ya utaarabu na lugha ya kitaaluma. Hivyo uwezo wao wa kudhibiti matumizi ya lugha kwa kututoa katika matumizi ya lugha mama yamefanikisha kuelekeza fikra za wanajamii hawa kwenye mawazo kwamba taaluma na usomi ni kujua Kiingereza.
              iii.            Kwa mujibu wa King’ei (2010) lugha hulejelea mazingira ya jamii husika, na ndiyo maana watu wenye lugha sawa na wanaishi katika mazingira tofauti wanaweza kuwa na mtazamo tofauti ya kimaisha na ufasili wao wa ulimwengu 
        iv.            Kwa kutumia nadharia ya ‘ukiliaji wa kiisimu’ (Linguistic Determinism) lugha ndiyo inayoongoza mawazo ya watu na huathiri hata maana ambazo watu wanazitoa kuelezea dhana na mitazamo fulani katika lugha zao.
           v.            Kwa njia ya lugha watu wa jamii Fulani wanapata nafasi ya kujadili masuala mbali mbali yanayohusu maendeleo ya jamii.
          vi.            Kama hiyo haitoshi, Austin (1962) anasema kuwa, ni muhimu kuhusisha matumizi ya lugha  na muktadha wake wa kijamii kwani lugha huwa na matumizi tofauti kama kutoa mapendekezo, kuahidi, kukaribisha, kuomba, kuonya, kufahamisha, kuagiza, kukashifukusifu, na kuapiza.
          vii.            Lugha ndicho chombo kinachotumika kuwaleta pamoja na kuwaunganisha wanajamii hukuikisaidia kuimarisha uhusiano miongoni mwa wanajamii. Katika muktadha wa Kiafrika, kwa mfano, heshima ya mtu inatambulishwa na jamii ya watu ndiyo maana waswahili wana msemo unaosema “mtu ni watu”. Kauli hii kwa ujumla inatuonesha kuwa katika harakati za maisha za wanajamii heshima na kukubalika kwa mtu pamoja na kueleweka kwake kunatokana na namna mtu anavyohusiana na wanajamii wengine pamoja na mambo mengine ikiwa ni kutumia lugha kwa ufasaha. Haya yote yanawasilishwa kutoka katika jamii moja kwenda katika jamii nyingine kwa kutumia lugha ambacho ndicho chombo muhimu cha mawasiliano.
        viii.            Jamii hutambulika kwa kutumia lugha. Lugha huwa na uwezo wa kuonesha sifa fulani kuhusu mzungumzaji, anayerejelewa na uhusiano uliopo kati ya wanajamii. Utamaduni hutambulishwa katika maeneo mbali mbali ya ulimwengu kwa kutumia lugha pia. Kwa mfano, katika fasihi ya kabila la Wahaya, tunatambua mambo mbali mbali yanayohusu kabila hili hasa katika kipengele cha majigambo kutokana na namna wanajamii hawa wanavyotumia lugha yao kujipambanua kwa jamii nyingine.
                ix.            Lugha pia hutumika katika kurithisha mila na desturi za jamii ikiwa na pamoja na kutolea elimu. Binadamu huweza kufunzwa na kupewa maadili mbali mbali kwa kutumia lugha ili waweze kujitambua kuwa wao ni akina nani na wapo ulimwenguni kwa malengo gani. Kwa mfano, watoto huwezwa kufunzwa masuala yanayohusu uana wao ambao hutokana na jinsia yao.  Kwa kutumia lugha. Pamoja na kuwa wanajamii wanaona matendi yanayotendwa na jamii nyingine au ndani ya jamii hiyo lakini wanahitaji namna ya kuambiwa juu ya uzuri au ubaya wamatendo hayo, kufuata au kuto yafuata. Hapa lugha inachukua nafasi yake.
   Marejeo
   King’ei, K. (2010). Misingi ya Isimu Jamii. Taasisi ya Taaluma za Kiswahili: Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Tanzania.

     Austin, J.L. (1962). How to do things with Words. Oxford. Oxford University Press.