Ijumaa, 26 Agosti 2016

KISA CHA BAO.

KISUMBUA KICHWA Na SALUMU CHIVALAVALA.
KISA CHA BAO.
Niwakumbushe kuhusu ya kale, kipindi ambacho paka alipokufa tulimzika njia panda huku tukiacha fagio pembezoni mwa kaburi lake ili kila apitaye asiache kufagia, kaburi la paka lilidumu kuwa safi siku zote. Na ni katika kipindi hicho hicho ambapo tulicheza bao kwa mtindo wa kula, kusafiri na hata kutakata.
Mpumbavu katika umri wa miaka arobaini ni mpumbavu wa milele, mimi sitaki hata kukaribia huko kabla ya kuondoa kila chembe ya upumbavu akilini mwangu. Nasema hivyo kwa sababu kupindua misingi ya kale ya kimaadili si kitu chema hata kidogo.
Wapo vijana wa rika yangu nilikuwa nao katika mti wa kivuli udondoshao majani ya aina mbili yaani ya kuwasha na ya kulainisha, tukiwa pale tulisimuliana kuhusu bao, nilieleza uzuri wa bao na hasa mchezo ukikuendea vema ukamla mwenzako mara kwa mara. Bao ni mchezo wa mababu na tumeukuta hivyo sie vijana. Ukicheza kwa ustadi na akili utakula sana kila tundu lenye kete nyingi na mwishowe utajizalishia kete nyingi katika majumba yako.
Wenzangu walinidhihaki kwa kusema bao la vijana huliwa mbele na nyuma hivyo niachane na mitindo ya kale, nikauliza “mbele na nyuma walaje!” nikaambiwa “ Muda huo huo wa kuchezwa ukifika hatua ya kula basi unakomba tundu la mbele na la nyuma huachi kitu aisee” nilistaajabu ya Musa ndio maana niliyaona ya firauni.
Kwa uchezaji huo kwakweli ni uharibifu tupu, kwa sababu mchezo wa bao kwa wachezaji hutumia vitobo vya nyuma kuhifadhi mitaji ya kete zao na kwa lugha rahisi tunaweza sema kule nyuma ndiko kunakowekezwa nguvu za mchezo, sasa ikitokea mtu anakula hadi huko basi ni wazi kuna uharibifu mkubwa wafanyika na haiwezi kutokea kukazaliwa kete nyingine kwa aliyeanza kuliwa bali mlaji ndio anaweza kuwa na uwezo wa kuzalisha kete kadiri atakavyo japo vidole vitachoka kwa ugumu wa kuvipeleka hadi nyuma kutafuta ulaji.

Kwa kuwa mjumbe hauawi, basi nami nasema jamani bao tucheze kama zamani, tule matundu ya mbele tupu tena tusiache kutakata kabla ya kula. Tukifanya hivyo tutajikuta tukifurahi siku zote na wala vidole hutakuta vikichoka mapema na wala hatutaharibu matundu ya nyuma yakabaki tupu kama fuko la mashine ya kusaga dona. Tuache mitindo ya nje iso na tija!