HISTORIA FUPI YA USHAIRI WA KISWAHILI
1.0
Utangulizi
Kiswahili
ni neno linayowakilisha dhana ya lugha iliyo na asili ya Kibantu, hususan lugha
zilizo katika mwambao wa Pwani ya Afrika Mashariki. Kwa mujibu wa Massamba
(2007), Kiswahili ni matokeo ya mkutaniko (convergence) wa jamii zilizokuwa
zinatumia lugha zenye asili ya Kibantu zilizojikuta katika upwa wa Afrika ya
Mashariki baada ya mtawanyiko (divergence) wa miaka mingi. Kwa hiyo, Kiswahili
kikawa ni matokeo ya mkutaniko huo wa jamii zenye asili moja[1].
Licha ya athari za wageni mbalimbali waliofika katika maeneo ya Waswahili
katika pwani ya Afrika Mashariki, lugha ya Kiswahili imebakia kuwa na tanzu
zake za kifasihi, hususan katika usimulizi. Utanzu mkongwe kuliko zingine ni
ushairi. Ushahidi wa kihistoria unaonyesha kuwa ushairi wa Kiswahili ulikuwapo
karne nyingi kabla ya kuja kwa wageni katika pwani ya Afrika Mashariki. Ushairi
huu ulikuwepo sambamba na Waswahili wenyewe, lakini ulikuwa katika hali ya
usimulizi. Tungo za Fumo Liyongo[2] ni
miongoni mwa ushairi wa zamani wa Kiswahili katika upwa wa Afrika Mashariki.
Kabla ya kuja wageni, hasa Waraabu, Waswahili walikuwa wakijulikana kwa majina
ya jamii zao za asili za kibantu kama vile Walamu, Wapate, Wapemba, Wadigo,
Wavumba, Waunguja, Wangazija na kadhalika. Ushairi wa jamii hizi uliendelea
kuwa katika hali ya usimulizi mpaka wageni kutoka nje ya bara la Afrika
walipoanza kuja. Kihistoria, tungo za fasihi ya Kiswahili hususan ushairi
zilihifadhiwa katika hati ya Kiarabu[3].
2.0 Historia ya Ushairi
Utanzu
wa ushairi ni utanzu ambao una historia ndefu miongoni mwa tanzu zote za
kifasihi. Hili ni kutokana na misingi kwamba, binadamu ana masuala mengi ya
kisaikolojia na kisosholojia ambayo mara nyingi humsumbua. Binadamu hujiona
razini na mwenye kipawa cha ubunifu kuliko wanyama wengine. Ndiposasa kila mara
yumo katika pilikapilika za kubuni mikakati mipya ya kukabiliana na mazingira
yake yanayobadilika kwa kasi mno.
Ushairi kama utanzu wa fasihi ya Kiswahili una historia tawili
ambayo hadi sasa tarehe kamili ya chanzi chake imegubikwa katika utata. Wallah
(1988) ana maoni kwamba licha ya utata huu, watafiti wengi wanakubaliana kwamba
ushairi huu ulianza pindi tu mwanadamu alipoanza kutumia nyimbo katika kazi
zake kama vile uvuvi, ususi, ukulima na uvunaji. Jamii za Kiswahili na za
Kiafrika kwa ujumla zilidumisha ushairi wao kupitia kwa masimulizi ya mdomo na nyimbo.
Vipengele vya lugha vilivyotawala ushairi huu wa Kiswahili aidha ni vya jadi
kama ulivyo ushairi wenyewe. Mojawapo ya hivi vipengele vya fani ni umbo na
sitiari.
3.0
Mihula ya Ushairi wa Kiswahili
Kezilahabi (katika Fasihi III,
1983) amegawa historia ya ushairi wa Kiswahili katika mihula minne ambayo ni;
Muhula wa Urasimi, Muhula wa Utasa, Muhula wa Urasimi Mpya na Muhula wa Sasa.
3.1
Mhula wa Urasimi
Ni vigumu kueleza ni lini hasa
mashairi ya Kiswahili yalianza kuchukua umbo lake la kimapokeo. Ni vigumu zaidi
kusema lini shairi fulani lilianza kuonekana katika hali ya maandishi. Tatizo
hili linasababishwa na kuwako kwa mashairi hayo katika hali ya fasihi simulizi
karne nyingi kabla ya hati za Kiarabu kufika upwa huu wa Afrika Mashariki.
Wakati mwingine matukio yatajwayo huweza kumsaidia mchunguzi kwa baadhi ya
maandishi, hasa yale yenye athari kubwa ya Kiarabu, huwa vigumu kusema kama
mwandishi aliandika kwa uasili wake mwenyewe au alikuwa akijaribu kukumbuka
shairi fulani la huko alikotoka. Hili bado ni jambo la kufanyiwa uchunguzi kuhusu mashairi ya zamani.
Kimaandishi
mashairi ya zamani yajulikanayo sana ni Utenzi
wa Tambuka (1728) ulioandikwa na bwana Mwengo, Utenzi wa Hamziya (1949) au
(1690) ulioandikwa na Sayyid Abdarus, Utenzi
wa Al-Inkishafi (1810 – 1820) ulioandikwa na Sayyid Abdallah A. Nasir na Utenzi wa Mwanakupona ulioandikwa na Mwanakupona mwenyewe. Tarehe za kuandikwa
kwa tenzi ni za kukisia, lakini kwa jumla ziliandikwa katika karne ya kumi na
nane na nusu ya kwanza ya karne ya kumi na tisa. Kimaandishi Utenzi wa Al-Inkishafi ni utenzi wa
kwanza wenye uzito kujadili matatizo na mazingira yaliyohusu Afrika ya Mashariki
na utenzi wa kiwango cha juu kabisa katika falsafa ya dini na wa kiwango cha
juu kisanaa. Ni utenzi wenye uasili japo hapa na pale unarejea katika Korani. Utenzi wa Hamziya ndiyo umetumia lugha
ya zamani kuliko tenzi zingine. Lugha iliyotumika ni Kingozi lakini ni tafsiri
ya utenzi wa Kiarabu ujulikanao kama “Kasidatul
Hamziya” ulioandikwa na Muhamed bin Said al-Busiry wa Misri. Hii ndiyo
tafsiri ya zamani ya kwanza kufanywa katika lugha ya Kiswahili tuliyonayo. Utenzi wa Mwanakupona (1858) ndio utenzi
pekee wa zamani ulioandikwa na mwanamke na ukaacha athari kubwa katika maisha
ya ndoa katika pwani ya kaskazini. Utenzi mwingine unaostahili kutajwa hapa ni Utenzi wa Fumo Liyongo (193?). utenzi
huu ndio utenzi pekee wa zamani wenye athari chache za nje. Ni utenzi wa
Kiafrika zaidi. Ni vigumu kusema kama kweli Fumo Liyongo alikuwa mshairi. Hili
bado ni jambo la kufanyia uchunguzi. Anayejulikana ni Fumo Liyongo wa
kihistoria aliyenyang’anywa ufalme wa Shagga na Daudi Mringwari. Zipo nyimbo
hapa na pale ambazo zimeitwa zake bila kuchunguza kama kweli kimtindo na
kimaudhui zinaweza kuwa zimeandikwa na mtu mmoja na katika wakati aliopata
kuishi. Nyimbo hizo ziliandikwa na mwandishi wa Utenzi wa Al-Inkishafi.
Tenzi
nyingine ni Utenzi wa Ayubu, Utenzi wa
Ngamia na Paa, utenzi wa Masahibu, Utenzi wa Kiyama, Utenzi wa Mikidadi na
Mayasa, Utenzi wa Ras al-Ghuli na Utenzi wa Shufaka. Hizi ni tenzi za
zamani ambazo hazisomwi sana siku hizi.
Upande
wa mashairi, kimaandishi mshairi aliyejulikana sana ni Muyaka bin Haji (1776 –
1940) na Bwana Mataka na Ali Koti. Wapo washairi wengine waliokuwa wakiandika
wakati huu lakini mashairi yao bado hayajakusanywa na kuwekwa katika hali ya
vitabu. Washairi hawa walifuatiwa na Muhammad Kijumwa na Hemedi Abdallah. Hapa
tunaweza kusema kuwa ndio mwisho wa muhula wa Urasimi katika fasihi ya
Kiswahili. Ni dhahiri kuwa kuhusu muhula huu uchunguzi mdogo sana umefanywa
sehemu ya upwa wa Kusini chini ya Tanga. Hemedi Abdallah ndiye mwandishi pekee
anayejitokeza.
3.2
Mhula wa Utasa
Miaka kati ya 1885 – 1945 tunaweza
kusema kuwa ulikuwa muhula wa utasa katika fasihi ya Kiswahili. Maandishi
machache yaliandikwa wakati huu, mengi yakiwa maandishi ya Hemedi Abdallah.
Tunapata pia Utenzi wa Vita vya Maji Maji
na Utenzi wa Vita vya Uhuru.
Kihistoria sababu zinajulikana. Ulikuwa ni wakati ambao mataifa ya Ulaya
yalikuwa yakigawana Afrika, vile vile wakati wa vita vya Dunia. Kimaandishi
ulikuwa wakati wa kubadilisha hati za maandishi. Mambo haya yalisimamisha
fasihi andishi ya Kiswahili kwa muda. Kwa hiyo kanuni za uandishi wa mashairi
zilianza kupotea.
3.3
Mhula wa Urasimi Mpya
Miaka ya 1945 – 1960 tunaweza
kuuita muhula wa urasimi mpya. Kazi kubwa ilikuwa ni kufufua kanuni hizi. Huu
ndio ulikuwa wakati wa Shaaban Robert, Amri Abedi, Khamis Amani (Nyamaume),
Mathias Mnyampala, Ahmed Nassir, Mdanzi Hanasa, Kibwana, Abdi Matunga, M.M.
Kihere na wengine wengi. Kwa hiyo kitabu
cha Sheria za Kutunga Mashairi kiliandikwa wakati ambao kilikuwa kinahitajika
sana ili kuweka kiungo kizuri na wakati uliopita. Lakini kwa sababu fulani
fulani muundo ulioshika sana ni muundo wa mizani 16 na katika mistari minne,
muundo uliotumika sana na Muyaka bin Haji katika karne ya kumi na nane. Sababu
mojawapo kubwa ni kuwa wanamapokeo waliamini kuwa shairi liliandikwa ili liimbwe,
wakati huo mghani Radioni Athumani Khalfani alikuwa amezoea kuimba mtindo huo
na katika mahadhi ya aina moja. Sababu nyingine ni kutopatikana kwa maandishi
ya amani hadi kamati ya Kiswahili ya Afrika Mashariki ilipoundwa. Shaaban
Robert ndiye aliyejaribu kutumia mitindo mbalimbali ya wakati uliopita.
Miaka
ya 1960 – 1967 ilikuwa miaka ya kuyumbayumba katika ushairi wa Kiswahili. Hii
ilisababishwa na nchi za Afrika Mashariki kutokuwa na malengo maalum baada ya
uhuru. Ulikuwa pia ni wakati ambapo washairi wawili mashuhuri walifariki. Hata
hivyo ulikuwa wakati ambao washairi wapya walikuwa wakijengeka.
3.4
Mhula wa Sasa
Miaka 1967 hadi leo tunaweza kuuita
muhula wa sasa. Kwa Tanzania ndio wakati wa kutafuta uhuru kamili katika lengo
la kufikia ujamaa. Washairi wengi walianza kuwa na mtazamo mpya kisanaa,
mgogoro juu ya kanuni za usahiri uliongezeka. Hapa lazima tujiulize, kwa nini
mgogoro huu unatokea katika muhula huu kwa nguvu zaidi? Swali hili limo katika
mkondo ule ule wa uhuru wa kiuchumi, uhuru wa kiutamaduni n.k. Kihistoria,
swali la uhuru katika ushairi linafuata mkondo huu wa uyakinifu wa kihistoria.
Ni tukio ambalo haliwezi kuepukika. Ni tukio muhimu katika historia ya ushairi
wa Kiswahili.
4.0
Maoni Mengine
Tunaweza kukubaliana au kutokubaliana
na mawazo ya Kezilahabi juu ya mgawanyo wa mihula kuhusu historia ya ushairi.
Kama ilivyoelezwa na wataalamu wengine kuwa ushairi wa Kiswahili hauna tarehe
maalum ya lini ulianza. Tunakubaliana na mawazo ya wengi kuwa ushairi wa
Kiswahili ulianza pale tu binadamu alipoanza kutumia lugha katika kujikimu
kimaisha. Na hivyo, ili kuielewa historia ya ushairi huu sharti tuuhusishe na
historia ya mswahili mwenyewe. Suala la kuwepo ama kutokuwepo kwa Waswahili
haliwezi kuchukua mjadala kwani lilikwisha kujadiliwa na wengi na kufikiwa
mwafaka. Hapa tutachunguza tu safari ya mabadiliko ya waswahili kutoka kwenye
hatua za mwanzo za kimaisha hadi kufikia hatua waliyomo sasa.
4.1
Ushairi wa Kiswahili Kabla ya Ujio wa Wageni
Katika hatua za mwanzo kabisa,
waswahili kama walivyo watu wengine wa mataifa na makabila mengine, waliishi
maisha ya ukusanyaji wa matunda, mizizi na uwindaji wa ndege na wanyama
wadogowadogo kwa ajili ya chakula. Baada ya kupiga hatua kidogo katika maisha
walianza kulima na hatimaye kufuga baadhi ya wanyama na ndege. Wakati
wakiendelea na shughuli zao hizo, fasihi yao hasa ushairi, ilifanya kazi kubwa
ya kuwahamasisha katika shughuli zao. Kwa hiyo, ushairi wa wakati huo ulikuwa
ni nyimbo za kazi, kubembelezea watoto na nyingine. Kila hatua ya maendeleo
waliyopitia waswahili na ushairi wao haukuachwa nyuma. Kadiri walivyozidi
kubadirika ndivyo ushairi nao ulivyobadirika na kuchukua dhima mpya. Mwanzo
kabisa dhima ya ushairi ilikuwa ni dhima za kiuchumi na kijamii. Baada ya jamii
kuingia katika matabaka na ushairi nao ukawa na dhima hizo za kitabaka. Kwa
muda mwingi zaidi ushairi wa Kiswahili ulikuwa simulizi kwa sababu waswahili
hawakujua kusoma na kuandika.
4.2
Ujio wa Waarabu
Ujio wa Waarabu ulileta athari
kadhaa katika ushairi wa Kiswahili. Athari kubwa ya kwanza ni kutambulishwa kwa
hati za kiarabu. Waarabu walipokuja katika upwa wa Afrika mashariki walianza
kuandika mashairi yao kwa Kiswahili kwa kutumia hati za kiarabu. Hapa ndipo
tunanza kupata ushairi andishi wa Kiswahili. Waarabu waliwafunza waswahili
kusoma na kuandika kwa kutumia hati za kiarabu. Waswahili nao walianza
kuhifadhi mambo yao katika maandishi kwa kutumia hati hii ya kiarabu.
Ushairi wa kale zaidi tunaoukuta
katika maandishi ni nyimbo za Fumo Liyongo. Kuja kwa Waarabu kunatambulisha
migongano kati ya ustaarabu na ushenzi (ukafiri). Hata hivyo Waarabu walifanya
juhudi kubwa ya kuwafundisha Waswahili ustaarabu wao kwa kuwasilimisha na
kuwafundisha dini. Hapo pia tunashuudia kukua kwa miji ya Waswahili ambapo
migongano inachukua nafasi kubwa zaidi, kati ya ushamba na umji.
4.3
Uvamizi wa Wareno
Kipindi cha miaka ya 1500 hadi 1730
kilikuwa kipindi cha Wareno kuvamia Pwani ya Afrika Mashariki, ambapo waliteka
miji ya Mombasa na Kilwa/Malindi. Ushairi wa kipindi hiki ulihusu migongano
kati ya wazungu na wenyeji. Ulikuwa ni mgogoro kati ya Ukristo na Uislamu.
Tenzi nyingi zilitungwa kipindi hiki lakini zaidi zilikuwa za kidini hasa
kupinga Ukristo. Baadhi ya tenzi hizo ni Herekali, Tambuka na Hamziya ambao
ulikuwa ni utenzi uliosimulia maisha ya mtume Mohamed, nao una mgogoro wa
kupinga Ukristo. Kuna wimbo ulioelekezwa kwa mzungu aliyeitwa Miguel (jina la
Kireno) kupinga mauaji aliyoyafanya dhidi ya Waswahili.
Mzungu
Migeli u mwongo
Mato
yako yana chongo
Kwani
kuwata mpango
Kwenda
kibanga uwani?
(Mulokozi
na Sengo, 1995:76)
4.4
Utawala wa Waoman
Kushindwa kwa Wareno mwaka 1730,
kuliwaweka Waswahili chini ya utawala wa Waoman baada ya wareno kuondoka, miji
iliyotawaliwa ni Zanzibar na Mombasa. Historia ya Waswahili inajikita katika
utawala wa Waoman. Washairi wanaojipambanua hapa ni Muyaka bin Haji na washairi
wa Pemba kama vile Kibabina, Ali Koti na wengine. Ushairi wa wakati huu ulihusu
mgogoro kati ya Waarabu na Waswahili. Pia kuna mgogoro kati ya mji na mji kama
vile Pate na Lamu, mmgogoro kati ya dini na siasa.
Muyaka bin Haji anaposema,
Jifungetoni
masombo,
Tuje
tuteze nao,
Bebeni
tezi na ngao, n.k,
Alikuwa akiwaasa Waswahili kuwa tayari kupambana
dhidi ya utawala kandamiza wa Waarabu.
Washairi wengine wanaoibukia katika
kipindi hiki ni Sayid Abdallah bin Ali bin Nassoro ambaye anatoa ya dini na
mtazamo wa Uislamu, anachora miji iliyoporomoka kutokana na athari za wareno –
Wakristo. Mwingine ni Mwanakupona binti Musham. Yeye anaibuka na mseto wa
utamaduni. Anafundisha malezi ya mwanamke, lakini bado ni utenzi ulioelemea
zaidi kwenye dini.
4.5
Ujio wa Wazungu
Mwishoni mwa karne ya 19, upwa wa
Afrika Mashariki ulivamiwa na kutawaliwa na Wazungu ambao walileta athari kubwa
katika ushairi wa Kiswahili. Kwanza kutambulishwa kwa hati za kirumi ambapo
Waswahili walianza kutumia hati hizo kuandika kazi zao. Ushairi kwa kipindi
hiki zaidi umejikita katika kupinga ukoloni. Miongoni mwa washairi
wanaojipambanua hapa ni Hemed bin Abdallah (1850 – 1928) aliyekuja na tungo za:
Utenzi wa Seyyidina
Hussein bin Ali (EALB, 1972)
Utenzi wa
Abdirrahamanni na Sufiyani (EALB, 1961)
Utenzi wa Kadhi Kassim
bin Jaafar (TUKI, 1974)
Utenzi wa Vita vya
Wadachi Kutamalaki Mrima (EALB, 1960)
Kazi nyingine zinazopatikana katika
kipindi hiki ni Utenzi wa Vita vya Majimaji. Kazi nyingi zaidi katika kipindi
hiki zilihusu maisha ya Washahili chini ya Ukoloni, watu waliojipendekeza kwa
wakoloni, wale waliopinga ukoloni, pia yaliibuka mashairi yaliyohusu maadili.
Baadaya kama miaka ya 1930 – 1960
kilikuwa kipindi cha mzinduko wa kitaifa na kitamaduni. Washairi katika kipindi
hiki walianza kutetea Uafrika. Mashairi mengi yaliyoandikwa katika magazeti ya
mambo leo yalihusu zaidi utamaduni na utu wa Mwafrika. Washairi kama vile
Shaaban Robert wanaibuka na kutetea Kiswahili. Shaaban Robert anawahimiza watu
wajiunge na chama cha TAA. Washairi wengine ni Mdanzi bin Hanasa, Swalehe
kibwana, Mwalimu Mwalimu Kihere na wengine..
Miaka ya 50 kilikuwa ni kipindi cha
mwamko wa kisiasa. Baada ya kutetea maadili wanavuka na kuanza harakati za
kumwondoa mkoloni. Kipindi hiki washairi walitumia mafumbo zaidi. Washairi
wanaojipambanua katika kipindi hiki ni Shaaban Robert, Amri Abedi, Saadan
Kandoro na wengine. Kandoro anamwandikia mjomba wake Amri Abedi aliyekuwa
anasoma Pakstani akimweleza harakati zilizokuwa zikiendelea huku nyumbani za
kumwondoa mkoloni. Miongoni mwa mashairi hayo ni pamoja na: Siafu wamekazana,
ondoka nchini kwetu, kwetu ni kwao kwa nini? Waafrika njooni na mengine mengi
yanayopatikana katika Mashairi ya Saadan. Sifa kubwa ya mashairi ya kipindi
hiki ni kupinga ukoloni.
4.6
Baada ya Uhuru
Baada ya nchi za Afrika Mashariki
kujipatia uhuru wake, Waswahili walikuwa kwenye shere za kushangilia uhuru.
Washairi nao hawakubaki nyumba kuimba nyimbo za kushangilia uhuru. Baadhi ya
mashairi yanayopatikana katika kipindi hiki ni pamoja na: Kujitawala, Chukua
hicho kiti na mengine. Mashairi yaliyotawala kipindi hiki ni ya kutafakari
Uhuru, mashairi ya kujenga taifa. Washairi wanaojipambanua zaidi hapa ni
Kandoro, (Kujitawala kugumu tujikongoje) na Nyerere (Usawa wa Binadamu na Chombo
cha Taifa Letu).
Katika harakati za kujenga taifa,
kulianzishwa siasa ya Ujamaa na Kujitegemea, falsafa iliyotokana na kutangazwa
kwa Azimio la Arusha mwaka 1967. Washairi nao wakasimama kuiimba siasa ya
ujamaa na kujitegemea. Mashairi yakaanza kuzungumzia ujamaa, ukombozi wa Afrika
na Azimio la Arusha. Baadhi ya kazi za kipindi hicho ni pamoja na:
Matunda ya Azimio
Malenga wa Bara
Miaka kumi ya Azimio na mashairi
mengine.
4.7
Mgogoro wa Ushairi
Kipindi cha miaka ya 1960 hadi 1970
jamii ya waswahili iliingia katika mgogoro mkubwa ambao uligawa washairi katika
makundi mawili. Ni kipindi ambacho nchi ilikuwa katika mabadiliko ambapo baadhi
ya watu walielekea kukata tamaa baada ya ahadi nyingi zisizotekelezeka. Sanaa
ya ushairi nayo ilikubwa na wimbi hili la mabadiliko na kuanza kuihakiki jamii.
Jambo kubwa lililotawala kipindi hiki katika sanaa ya ushairi ni kuwa mashairi
yaweje? Baada ya wananchi kuanza kukata tamaa na wengine kuona ujamaa unasalitiwa,
wakaanza kuuhakiki ujamaa. Miongoni mwa washairi wanaojitokeza katika kuuhakiki
ujamaa ni pamoja na E. Kezilahabi, Mulokozi na Kahigi.
4.8
kKipindi cha Sasa
Kezilahabi na diwani yake ya Dhifa
anatuingiza katika kipindi cha sasa ambapo uhuria umetawala. Watu wanagawana
mali ya Umma, watu wako kwenye dhifa wanagawana mali ya nchi wanakula.
5.0
Maendeleo
Katika kipindi cha sasa twaweza
kuona kuwa idadi ya washairi imeongezeka, idadi ya mashairi imeongezeka na
ubora wa mashairi umeimarika. Ushairi leo unashirikisha watu wengi zaidi hasa
baada ya kufundishwa shuleni. Mabadiliko ya 1960 yamezua fani mpya kama vile
ngojera na sasa ushairi umekuwa sanaa ya umma. Kumekuwa na:
i.
Mashairi huru mengi
ii.
Mashairi ya kidrama
iii.
Ushairi wa vijana
(Bongo Flever) unaosaili yaliyopo
iv.
Ushairi unabadilika
kuendana na hadhira, wanachanganya ushairi na ngoma.
6.0
Matatizo
Pamoja na mafanikio hayo katika
ushairi wa Kiswahili bado pana matatizo mengi ambapo leo:
i.
Kuna matatizo katika
masuala ya uchapishaji
ii.
Diwani siyo nyingi
iii.
Magazeti si mengi yenye
kutoa kurasa za mashairi kama zamani
iv.
TV na Redio hawawapi
nafasi za upendeleo washairi.
[1]
Rejelea katika Massamba 2007
[2]
Fumo Liyongo ni shujaa katika historia ya Kiswahili ambaye tungo zake
zinasemekana ni za zamani sana, na
aliishi katika upwa wa
Afrika Mashariki.
[3]
Waarabu ndio wageni walioiita pwani ya Afrika Mashariki kwa jina la sahel, na wenyeji wake kuitwa wasuahel. Hili ndilo jina walilopewa
wenyeji wa pwani kama Waswahili,
yaani wenyeji wa pwani, na huu ndio mwanzo wa matumizi ya neno Waswahili. Aidha lugha yao iliitwa Kiswahili.
+++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++
Kiswahili na TEHAMA
MAENDELEO YA KISWAHILI
KATIKA TEKNOLOJIA YA HABARI NA MAWASILIANO (TEHAMA)
Aritamba Malagira
Chuo Kikuu Cha Dar es
Salaam
Ikisiri
Teknolojia ya habari na
mawasiliano imekuwa ikikua kila siku kutoka simu ya kukoroga hadi simu ya
mkononi, matumizi ya wavuti na nyinginezo nyingi, kwa kweli ni hatua kubwa ya
maendeleo katika teknolojia. Hivi sasa watu wanawasiliana ndani ya sekunde chache
kwa umbali wa kutoka bara hadi bara kupitia wavuti. Katika hali kama hii lugha
za ulimwengu nazo zimekuwa zikijitahidi kukabiliana na ukuaji huu wa teknolojia
kwa kutafuta istilahi mpya ili kuelezea dhana mpya za kiteknolojia zinazoibuka.
Katika harakati hizi, Kiswahili hakiko nyuma, istilahi mpya za Kiswahili
zimekuwa zikiundwa ili kukidhi haja ya kuwasiliana kupitia Teknolojia ya habari
na mawasiliano. Makala hii inalenga kuangalia hatua iliyofikiwa na Kiswahili
katika tasnia ya teknolojia ya habari na mawasiliano ikiwa ni pamoja na
kuchunguza istilahi za ki-TEHAMA zinazotumika.
1. Utangulizi
Teknolojia ya habari na
mawasiliano imekuwa kiungo muhimu sana katika maendeleo ya watu duniani. Watu
wamekuwa wakitumia teknolojia hii katika kufanya mawasiliano muhimu, kufanya
bishara na mambo mengine mengi yanayowanufaisha watu. Kompyuta/ Talakirishi ni
moja ya kifaa kilicholeta mapinduzi katika TEHAMA kama asemavyo Katambi (2011)
“Kompyuta amaTarakilishi katika lugha ya Kiswahili ni kifaa ambacho
kimebadilisha kabisa mfumo wa maisha ya binadamu katika miongo takribani sita
iliyopita. Kutokana na kuwapo kifaa hiki dunia imejikuta katika maendeleo
makubwa kabisa kuliko kipindi chochote kile katika historia ya kuwapo kwake.
Kifaa hiki kimeleta mabadiliko makubwa Sana katika maisha ya kawaida ya
binadamu. Kifaa hiki kimesababisha mambo mengi kufanyika katika hali ambayo
hakika isingewezekana au ambayo awali ingeonekana kama ya kufikirika!. Kompyuta
imeyafanya maisha kuwa rahisi zaidi. Kompyuta imeifanya dunia kuwa Kama kijiji
kidogo ambacho unaweza kukizunguka katika muda mfupi Sana wa sekunde chache”.
Maneno haya ya Katambi yanaonesha ni jinsi gani kompyuta ilivyo muhimi katika
TEHAMA, mawasiliano yote ya teknolojia ya habari hufanywa kwa kutumia kompyuta,
mfano; matangazo ya redio na televisheni, magazeti na n.k huandaliwa
kwa kutumia kompyuta na kuwa tayari kwa ajili ya kupasha habari.
Makala hii, kwa kuzingatia
umuhimu wa TEHAMA katika dunia ya sasa imejikita katika kuchunguza maendeleo ya
Kiswahili katika uga wa habari na mawasiliano kwa umahususi zaidi katika
mawasiliano yanayohusisha matumizi ya kompyuta hususani wavuti na programu
nyingine za kompyuta. Tutaangalia umuhimu wa matumizi ya Kiswahili katika
TEHAMA, maendeleo yaliyofikiwa, changamoto na mwisho ni hitimisho.
2. Usuli
Neno Teknolojia ya Habari
na Mawasiliano (TEHAMA) kwa ujumla wake hurejelea mifumo yote ya kiteknolojia
inayotumika kutengeneza, kuhifahdi, kuchakata na kutumia habari katika mifumo
yake tofautitofauti (data, picha, uwasilishaji wa medianuwai na mifumo mingine
mingi) na mabayo huwezesha, kurahisha na kutegemeza mawasiliano. Kwa umahususi
zaidi, TEHAMA inarejelea kukutana au kuingiliana kwa mikroelektroniki, talakirishi na
mawasiliano ya kutumia redio, simu au televisheni ambavyo hufanya kuwezekana
kwa data, ikiwa ni pamoja na matini, video na ishara za video kuweza
kusafirishwa mahali popote duniani ambapo ishara za kidijitali huweza
kupokelewa… (Howell na Lundall, wakinukuliwa na Akinyi 2010). Kwa ujumla TEHAMA
inahusu mambo mengi sana, matumizi ya kompyuta, wavuti, matangazo ya redio na
televisheni, satelaiti, picha na mambo mengine mengi yafananayo na hayo
hujumuishwa katika teknolojia ya habari na mawasiliano.
2.1 Umuhimu wa TEHAMA katika
maendeleo kwa ujumla
Teknolojia ya Habari na
Mawasiliano kwa ujumla imechangia sehemu kubwa kuleta maendeleo hasa katika
kipindi hiki cha karne ya 21 ambapo utandawazi umeenea ulimwengu mzima na
kuifanya dunia kuwa kama kijiji ambapo watu huwasiliana na kufanya kazi na
biashara kwa pamoja kama wapo katika kijiji kimoja, mambo haya yote
yanafanikiwa kwa kuwezeshwa na TEHAMA. Kama asemavyo Kamau (2009) kuwa
ushirikiano wa kimataifa katika mambo kama vile siasa, biashara, uchumi ,
michezo n.k huwezeshwa na kurahisishwa na teknolojia ya habari na
mawasiliano (TEHAMA) ambayo imeuunganisha ulimwengu mzima kimawasiliano. Kwa
maelezo haya tunaweza kuona ni jinsi gani TEHAMA ilivyo kuwa muhimu katika
ulimwengu wa sasa.
Lugha ni muhimu sana katika
suala zima la Teknolojia ya Habari na Mawasiliano hatuwezi kuhamisha maarifa
yaliyopo katika teknolojia hii bila kutumia lugha na kwa hiyo ili kuwapo na
maendeleo endelevu kupitia TEHAMA ni lazima pia lugha inayotumika kuhamisha
maarifa ya teknolojia hii iwe inaleweka kwa watumiaji husika. Hii itakuwa rahisi
kwao kuilewa na kuitumia teknolojia hii vilivyo kwa sababu lugha inayotumika ni
lugha wanayoifahamu na ni lugha yao.
Kama tujuavyo bara la
Afrika halijaendelea sana kwa kiwango cha kuzalisha teknolojia zitakazo
kubalika katika masoko ya kimataifa kama yafanyavyo mabara mengine hususani
mabara ya Ulaya na Marekani, kwa hiyo kulingana na hali hii Afrika imekuwa
ikiingiza teknolojia za kigeni kutoka Mabara mengine hasa Marekani na Ulaya,
teknolojia hizi zimekuwa zikiingizwa kwa lugha za kigeni jambo ambalo hufanya
watumiaji wengi wa Waafrika kushindwa kumudu matumizi ya teknolojia hizi kwa
sababu hawajui lugha iliyotumiwa. Kwa mfano kompyuta zinazoingizwa Afrika
programu zake huwa zimeandikwa kwa lugha za kigeni hususani kiingereza, watu
mabao wataweza kuzitumia kwa urahisi ni wale ambao wanazijua lugha hizi vilivyo
na kuwaacha wale wasiojua wakiwa wameduwaa ambao kimsingi ni wengi kuliko wale
wanaojua. Kwa hiyo, ili kuondokana na tatizo hili, upo umuhimu mkubwa wa
kuziendeleza lugha za Kiafrika kiteknolojia. Suala hili ni la msingi sana,
kwani kwa kufanya hivi hatutakuwa tumeendeleza lugha tu bali pia tutakuwa
tumeindeleza jamii yetu kiteknolojia.
2.2 Kwa
nini Kiswahili katika TEHAMA
Wataalam wengi wanipigia
upatu lugha ya Kiswahili kuwa lugha ya utandawazi barani Afrika, hii ni kwa
sababu lugha ya Kiswahili imeendelea sana kuliko lugha nyingine za Kiafrika na
ndiyo lugha pekee iliyoonekana kuwa tayari kupokea kwa haraka mabadiliko ya
kiteknolojia yanayoibuka kila siku duniani. Kwa maana kwamba lugha ya Kiswahili
ina utajiri mwingi wa msamiati kiasi cha kukabiliana na teknolojia za kigeni
zinazoibuka bila matatizo yoyote. Kama asemavyo Kamau (2009) “kwa vile
utandawazi huhusika na uunganishaji wa mataifa mbalimbali, basi Afrika yahitaji
lugha moja yenye asili ya Kiafrika kama lugha ya kusambaza utandawazi. Kwa sasa
mfano mzuri wa lugha kama hii ni lugha ya Kiswahili. Lugha hii ndio lugha
kutoka barani Afrika ambayo ina matumizi mapana kuliko lugha nyingine hapa
barani na kwingineko”. Nukuu hii inatuonesha ni jinsi gani lugha ya Kiswahili
ilivyo muafaka katika suala zima la utandawazi wa Afrika. Kimsingi utandawazi
husambazwa kupitia lugha na teknolojia, kwa hiyo tunaweza kuona jinsi lugha
ilivyo chombo muhimu sana katika maendeleo ya teknolojia na kwahiyo Kiswahili
kama lugha ya kiafrika ni muhimu iwe imejiendeleza na kujitosheleza
kiteknolojia kwaajili ya mahitaji ya watu wake.
Kutokana na umuhimu wa
TEHAMA kama ilivyofafanuliwa hapo juu na kutokana na umuhimu wa
lugha katika maendeleo ya kiteknolojia, tunaweza kuona jukumu la lugha ya
Kiswahili katika Teknolojia ya Habari na Mawasiliano. Lugha ya Kiswahili
imebeba jukumu kubwa la kuhakikisha wakazi wa Afrika Mashariki wanaipata na
kuitumia teknolojia mpya kwa lugha wanayoifahamu ambayo ni Kiswahili. Kwa
kufanya hivi matumizi ya teknolojia yataimarika katika ukanda huu wa Afrika
Mashariki. Kwa misingi hii naweza kusema ndio sababu pekee iliyonisukuma
kuichunguza lugha ya Kiswahili katika uwanja wa Teknolojia ya Habari na
Mawasiliano.
3. Hatua
iliyofikiwa na lugha ya Kiswahili katika TEHAMA
Kwa kweli lugha ya
Kiswahili imepiga hatuta kubwa sana katika Teknolojia ya Habari na Mawasiliano.
Kama tulivyo kwisha kusema huko awali kwamba TEHAMA ina uwanja mpana sana,
tunapozungumzia TEHAMA tunazungumzia vitu vingi sana kama vile matangazo ya
redio na televisheni kwa namna yanavyofanywa, matumizi ya kopmyuta kwa namna
yake n.k. Katika makala hii tutajikita zaidi katika matumizi ya kompyuta kwa
namna yake, tutajikita hapa kwani hii ndio inaonekana kuwa teknolojia mpya
kabisa katika mazingira ya lugha ya Kiswahili na dhana mpya zinazidi kuibuliwa
kila siku katika matumizi ya kompyuta.
Kompyuta kimekuwa kifaa
muhimu sana katika shughuli nyingi za kimaendeleo, kwa kutumia kompyuta watu
wamekuwa wakifanya mambo chungu nzima na kwa urahisi sana. Bila shaka umekwisha
sikia kuwa unaweza kununua bidhaa kwa kutumia kompyuta ukiwa nyumbani kwako
bila ya hata kwenda huko sokoni au dukani. Bila shaka umekwisha sikia kuwa
mabenki, hospitali, taa za kuongozea magari barabarani, kamera za usalama,
ndege za abiria na kivita na hata lift unazopanda kila siku unapoingia na
kutoka ofisini katika jengo refu huendeshwa kwa msaada wa kompyuta. Bila shaka
umekwisha jionea mwenyewe au kusikia habari kama hizi. Umekwisha sikia kuwa mtu
anaweza kumchagua mgombea wa urais au ubunge kwa kutumia kompyuta! Haya na
mambo chungu nzima hufanyika kwa msaada wa kompyuta. Katika nchi zilizoendelea
matumizi ya kifaa hiki yanaendelea kushika hatamu kiasi kwamba kila kitu sasa
kinafanywa Kwa kutumia mashine zinazoongozwa kwa kompyuta.
Kwa hiyo unaweza kuona ni
jinsi gani matumizi ya kompyuta yalivyokuwa muhimu sana katika maisha ya kila
siku. Serikali za Jumuia ya Afika mashariki zimekuwa zikisisitiza matumizi ya
kompyuta kuanzia shule za awali, kwa kuzingatia kwamba matumizi ya kompyuta
yameongezeka sana katika ulimwengu wa sasa lakini changamoto zinazoikabili
progaramu hii imekuwa ni lugha ya kufundishia. Kwa mfano Tanzania somo la
TEHAMA linafundishwa kuanzia shule za msingi; shule za msingi kwa Tanzania
hutumia lugha ya Kiswahili kama lugha ya kufundishia na kwa
kuwa programu za kompyuta zimeandikwa kwa kiingereza, italazimika programu hizo
zitafsriwe katika Kiswahili ili ufundishaji uweze kuwa rahisi. Na hapa ndipo
tunapata istilahi mpya za Kiswahili katika Teknolojia ya Habari na Mawasiliano.
Licha ya uhitaji wa
kufundishwa somo la Kiswahili katika shule za awali lakini pia makampuni
makubwa yanayohusika na mawasiliano ya kompyuta yamekuwa yakitafuta nija ya
kujiimarisha kibishara katika maeneo mbalilimbali duniani. Mbinu moja wapo
amabyo wemekuwa wakiitumia ni kuhakikisha wateja wao wanapata huduma kwa lugha
yao. Kwa mfano kampuni ya Microsoft kwa mara ya kwanza kabisa katika historia
ilianzisha mradi wa kutafsiri program zake kwa Kiswahili. Kama asemavyo King’ei
(2010) “kampuni ya talakirishi iitwayo microsoft ilitekeleza
hatua ya kihistoria mwaka 2005 kwa kuanzisha kamusi maalumu
inayowawezesha watumiaji wa talakirishi kutumia lugha ya Kiswahili katika
mawasiliano yao yote kwa kompyuta. Programu hii mpya inamwezesha mtumiaji
kompyuta asiyefahamu lugha nyingine kama vile kiingereza kutumia kompyuta na
kuwasiliana bila shida yoyote”.
Msanjila na wenzake (2011)
pia wanasema hadi wakati huu lugha ya Kiswahili imekwisha ingizwa katika mifumo
miwili ya kompyuta ijulikanayo kama linuksi na mikrosofti. Wanaendelea
kusema, kuingizwa kwa Kiswahili katika mifumo hii maana yake ni kwamba mtumiaji
anaweza kuvinjari mifumo hiyo ya kompyuta kwa Kiswahili akiamua kufanya hivyo.
Kwa mujibu wa maelezo ya
wataalamu hawa ni wazi kwamba mpaka sasa hivi Kiswahili kinatumika katika
baadhi ya mifumo ya kompyuta. Katika kufanikisha hili ujanibishaji wa programu
kadhaa za kompyuta ulifanyika. Kahigi (2007) anasema “Mradi wa ujanibishaji wa
Office 2003 na Windows XP kwa Kiswahili sanifu ulitekelezwa katika kipindi
2004-2005. Malengo ya maradi yalikuwa: (1) kuandaa istilahi za kompyuta kwa
Kiingereza-Kiswahili, na (2) kutafsiri programu nne za kawaida za Office
(Outlook, Excel, Word na PowerPoint) na Windows XP”. Hii inamaanisha kwamba
programu hizi zinapatikana katika lugha ya Kiswahili. Hebu tuangalie mifano ya
istilahi kutoka katika programu hizi za Office 2003 na Windows XP kama
zilivyoorodheshwa na Kahigi, ni istilahi zaidi ya 600 lakini hapa tutaangalia
chache tu:
1.
Fikia Access
2.
Kibonye fikishi Access
key
3.
Viziada Accessories
4.
Amilisha Activate
5.
Kirekebu Adapter
6.
Kihadharishi Alert
box
7.
Program matumizi Application
8.
Makaaba Archive
9.
Vitome mchoro Bit map
10.
Kiashiri mada Book
mark
11.
Sakura Browse
12.
Kisakuzi Browser
13.
Kwa
kaida By
default
14.
Msabidi Configuration
15.
Sabidi Configure
16.
Puna Crop
17.
Kielekezi Cursor
18.
Tanafsi Custom
19.
Pakua Download
20.
Kijachini Footer
21.
Nakala bayana Hard copy
22.
Kidakuzi Cookie
23.
Sanidi Install
24.
Kicharazio Keyboard
25.
Kiolezo Template
26.
Tafutatua Trouble-shoot
27.
Sanidua uninstall
28.
Sasaisha Update
29.
Kidhulishi Highlighter
30.
Kichapishi Printer
31.
Kingavirusi Antivirus
Hizi ni baadhi tu ya
istilahi kati ya nyingine nyingi zilizoundwa katika mradi wa kujanibisha
programu za office 2003 na Windows XP. Jitihada za kampuni ya Microsoft hazikuishia
hapo tu, mnao mwezi mei mwaka 2011 kampuni hii ilizindua programu ya Windows 7
kwa Kiswahili, hatua hii imezidi kukiimarisha Kiswahili katika Teknolojia ya
Habari na Mawasiliano. Haya ni maendeleo makubwa katika lugha ya Kiswahili. Kwa
hiyo sasa mtumiaji wa Kiswahili anachaguo la kufanya, ama kuendelea kutumia
programu hizi kwa lugha ya Kiingereza au kwa lugha ya Kiswahili.
4. Changamoto
zinazoikabili lugha ya Kiswahili katika Teknolojia ya Habari na Mawasiliano
Kila jitihada zinazofanywa
katika kufikia malengo fulani huwa hakukosi changamoto. Katika jitihada za
kufanya Kiswahili kuwa lugha ya kiteknolojia kumetokea changamoto nyingi, moja
wapo iliyo kuu kabisa ni kwamba lugha ya Kiswahili haimilikiwi na taifa lolote
tajiri kwa hiyo katika harakatika za kuendeleza inakumbana na changamoto nyingi
kama vile ukosefu wa fedha na hata utayari wa viongozi wa kisiasa kukiendeleza
Kiswahili ni mdogo sana, hata hivyo harakati hizi zinapingwa na mataifa ambayo
lugha zao zimeendelea sana kiteknolojia kwa kuhofia kwamba zitafunikwa na
matumizi ya Kiswahili. Wapo tayari kutoa misaada ili kuendeleza lugha zao
kukididimiza Kiswahili kitu ambacho kinafanya harakati za kukiendeleza
Kiswahili kuwa ngumu kwani nchi kinamozungumzwa Kiswahili hazina pesa za
kupambana na mataifa makubwa yanayopigia upatu lugha zao.
Kutokana na sababu hizo,
kasi ya uundaji wa istilahi za kiteknolojia imekuwa ndogo sana, kwani kufanya
hivyo pia kunahitaji pesa, na mara nyingi pesa zimekuwa zikitolewa na wahisani
au makampuni yanayohusika kitu kinachotokea mara moja baada ya muda mrefu sana.
Pia, viongozi wa serikali
hawajatilia mkazo suala hili, hawajaona umuhimu wa kukiendeleza Kiswahili
kitenolojia. Nguvu zao nyingi wameziweka katika miradi mingine ya kimaendeleo
huku wakisahau kabisa kuwa Kiswahili pia kinahitaji kwenda sambamba na
maendeleo hayo. Kwa hiyo hii imekuwa ni changamoto katika maendeleo ya lugha ya
Kiswahili.
Kwa kuwa istilahi hizi
zimekuwa zikifanywa na watu tofautitofauti, ni muhimu kuwapo na jopo
maalumu la kusanifisha istilahi hizi kabla hazijasamabazwa. Kwa kufanya hivi
hakutakuwa na matumizi tofauti ya istilahi katika dhana moja. Hali hii
inajitokeza sana endapo uundaji wa istilahi utakuwa umefanywa katika makundi
tofauti.
Utayari wa watumiaji;
watumiaji wengi wa lugha ya Kiswahili wamekuwa wakilalamika kuhusu kutumia
programu za komyuta kwa lugha za Kiswahili. Madai yao ni kwamba istilahi za
Kiswahili ni ngumu sana na hivyo si rahisi kuzitumia, kwa mfano, wengi wamezoea
kusema password na kwa hiyo ukiwaambi kwamba password kwa
Kiswahili huitwa nywila au mouse inaitwa pukuwatabaki
wakikushangaa na watona kama unawapa kazi kubwa sana. Kwa hiyo hii nayo
inasabaisha matumizi ya Kiswahili katika vifaa vya kiteknolojia hususani kompyuta
kuwa hafifu.
5. Hitimisho
Katika makala hii tumeona
TEHAMA ni kitu gani na umuhimu wake katika maisha ya kila siku ya binadamu,
tumeona umuhimu wa lugha za kiafrika kuendelezwa katika Teknolojia ya Habari na
Mawasiliano kwa umahususi zaidi tumeona jinsi Kiswahili kilivyo muhimu zaidi
katika uwanja wa maendeleo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano. Tumengalia
pia maendeleo yaliyofikiwa na lugha ya Kiswahili katika TEHAMA huku tukionesha
baadhi ya istilahi za Kiswahili zinazotumika katika matumizi ya kompyuta, pia
tumeangalia changamotozinazo ikabili lugha ya Kiswahili katika jitihada za
kuiendeleza kiteknolojia. Sasa tuangalie mapendekezo juu ya nini kifanyike ili
kuhakikisha lugha ya Kiswahili inashika hatamu katika Teknolojia ya Habari na
Mawasiliano:
Viongozi wa ukanda wa
Afrika Mashariki waungane kuhakikisha wanaunda sera nzuri kuhusiana na
maendeleo ya lugha ya Kiswahili ikiwa ni pamoja na kuandaa mradi maalumu wa
kuunda istilahi mbalimbali za kiteknolojia, hii itasaidia lugha ya Kiswahili kuimarika
katika matumizi ya teknolojia. Pamoja na hilo pia itenge bajeti maalumu kwa
ajili ya kuandaa na kutekeleza miradi mbalimbali ya kuunda istilahi za
Kiswahili katika teknolojia zinazoibuka ili kuahakikisha wazungumzaji wa lugha
ya Kiswahili hawaachwi nyuma katika matumizi ya teknolojia mpya ziibukazo.
Pia kutokana na changamoto
ya kutokuwapo na jopo maalumu la kuunda istilahi za kiteknolojia pindi mradi
kama huu unapotokea, hali hii imesababisha kuwapo kwa istilahi ambazo
hazijasanifishwa na pengine kuwapo na istilahi zaidi ya moja inayorejelea dhana
moja, hii ni kwa sababu miradi kama hii hufanywa na watu tofautitofauti na
pengine wataalamu hawa wana ujuzi katika lugha tu lakini katika teknolojia
hususani kompyuta hawana maarifa ya kutosha au hawana kabisa. Katika hali kama
hii ni vigumu kuunda istilahi zinazofanana au zinazobeba dhana kamili kama
ilivyokuwa ikikusudiwa katika lugha chanzi. Kwa hiyo katika uundaji wa istilahi
za kiteknolojia ni vema kuwepo na jopo maalumu amablo lina ujuzi wa kutosha katika
lugha na masuala ya kiteknolojia, hii itasaidia kutoa istilahi nzuri na
zinazoeleweka kwa urahisi kwa watumiaji.
Baada ya kuundwa istilahi
hizi inatakiwa zisambazwe kwa watumiaji kwa kiwango kinachoridhisha ili waweze
kujifunza na kuzifahamu na hatimaye kuzizoea katika matumizi yao ya kila siku
katika Teknolojia ya Habari na Mawasiliano. Nasema hivi kwa saba usambazaji wa
istilahi hizi umekuwa haufanywi kwa kiwango kinachohitajika, na katika
usambazaji, vyombo vya habari vipewe kipaumbele, kwani istilahi hizi zikitumiwa
na vyombo vya habari itakuwa rahisi sana kwa watumiaji wengine
kuzitumia.
Wazungumzaji wa Kiswahili
pia wawe tayari kutumia istilahi hizi au programu za Kiswahili katika matumizi
yao ya kopmyuta. Programu kadhaa za kompyuta zimejanibishwa kwa Kiswahili
lakini wazungumzaji wengi wa Kiswahili bado wanatumia programu zilizoandikwa
kwa lugha ya Kiingereza, program ya Windows 7 inapatikana kwa Kiswahili lakini
nina wasiwasi kama miongoni mwetu kuna mtu hata mmoja anayetumia Windows 7 ya Kiswahili.
Kwa hiyo napendekeza kwenu suala hili, kwa kuwa sisi tumejitoa kueneza na
kuienzi lugha ya Kiswahili pia ni jukumu letu kuchangamkia fursa kama hizi,
tuwe wa kwanza kutumia programu kama hizi kwa Kiswahili pindi zinapotokea, kwa
kufanya hivi tutakuwa tunakienzi Kiswahili na kukikuza kwani watu
wanaotuzunguka watakapotuona tunatumia Windows ya Kiswahili watashawishika na
wao kuitumia, hivyo kwa njia hii tutakuwa tumefanikiwa kukuza na kuienzi lugha
ya Kiswahili.
Ninaamini kila mmoja wetu
ana ndoto za kuona lugha ya Kiswahili siku moja inakuwa lugha ya bara zima la
Afrika, kwa maana kwamba Kiswahili kinazumgumzwa kila kona ya bara hili, basi
kama ndio ndoto zetu sote hatuna budi kupigania maendeleo ya lugha ya Kiswahili
kwa nguvu zetu zote, tukifanya hivi kwa pamoja kwa kijishughulisha na masuala
yanayohusika na Kiswahili, kwa kuandika, kufanya utafiti katika Nyanja
mbalimbali za lugha ya Kiswahili ndoto zetu zitatimia na kumbukumbu zetu
zitakumbukwa katika vizazi vinavyokuja kama anavyokumbukwa leo hii Shaaban
Robert. Ninaamini kuwa tunaweza!!
Kiswahili, Hazina ya Afika
kwa Maendeleo Endelevu!
Marejeo
Akinyi, J.J. (2010). Kiswahili usage in ICT in NEPAD
secondary schools in Kenya. Katika TheJournal
of Language, Technology & Entrepreneurship in Africa, Vol. 2.
No.1. www.ajol.info/index.php/kcl/article/vieFile
Kahigi, K.K (2007).
Ujanibishaji wa office na windows xp kwa Kiswahili sanifu.
Katika Kioo cha
Lugha juzuu la 5. Dar es salaam. TUKI.
Kamau, S.N. (2009).
Kiswahili, utandawazi na umoja wa Afrika. Katika journal of language,
technology& entrepreneurship in Africa vol.1.
www.ajol.info/index.php/kcl/article/vieFile
Katambi, S (2011). Teknolojia ya Habari na Mawasilianao
(TEHAMA). Dar es salaam:
Modecs Solutions
King’ei, K (2010). Misingi
ya isimujamii. Dar es salaam. Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili.
Msanjila,Y.P, Kihore,Y.M na
D.P.B Massamba (2011). Isimujamii sekondari na vyuo.
Dar es salaam. Taasisi ya
Uchunguzi wa Kiswahili.
Osborn, D. Z. (2006).
African Languages and Information and Communication
Technologies: Literacy,
Access, and the Future. Katika Selected Proceedings of the 35th
Annual Conference
on African Linguistics, ed. John Mugane et al., 86-93. Somerville,
MA: Cascadilla
Proceedings Project. www.lingref.com, document #1299.
Osborn, D. Z. (2010). African
Languages in a Digital Age. Cape Town: HSRC Press.
++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++
CHUO KIKUU CHA DAR ES SALAAM
TAASISI YA TAALUMA ZA KISWAHILI
IDARA YA LUGHA YA KISWAHILI NA ISIMU
KI113:MBINU ZA UTAFITI NA UANDISHI WA TASNIFU KATIKA
LUGHA NA FASIHI
RIPOTI YA UTAFITI KUHUSU MBINU ZILIZOTUMIKA
KATIKA UUNDAJI WA ISTILAHI ZA KISWAHILI ZILIZOINGIZWA KATIKA MIFUMO YA
MAWASILIANO YA KOMPYUTA: MIFANO KUTOKA MFUMO WA KOMPYUTA WA LINUX.
JINA: MALAGIRA ARITAMBA.
NAMBA YA USAJILI: 2010-04-02466
MWALIMU WA SOMO: E. MAHENGE NA DKT. G. MRIKARIA
SHUKRANI
Utafiti huu umefanikiwa kwa jitihada kubwa za waalimu wangu wa
somo.Napenda nimshukuru kwa dhati mwalimu Elizabeth Mahenge kwa kutumia muda
wake mwingi katika kunielekeza na kurekebisha mada yangu ya
utafiti.Namshukuru pia Mwalimu G.Mrikaria kwa kututia moyo katika kufanikisha
utafiti huu.
Vilevile nawashukuru wanafunzi wenzangu kwa kunishauri na kunitia
moyo katika kuendelea na utafiti huu.Wanafunzi wafuatao wamekuwa mchango mkubwa
katika kufanikisha utafiti huu;Ally Laila,Thomas Edson,Ndumbaro Eric, Ndege
Busalu pamoja na Ntenga Elias.Nawashukuru pia Boniface Jacob na James Balele
kwa utayari wao wa kunisaidia kuchapa utafiti huu.Na mwisho nawashukuru wote
walionisaidia kwa namna moja ama nyingine,Mungu awabariki sana!
.
YALIYOMO
Sura ya kwanza:Utangulizi na Nadharia ya uundaji istilahi………………….
1
1.0 Utangulizi……………………………………………………………………………………1
1.1 Tatizo la utafiti……………………………………………………………………….3
1.2 Malengo ya utafiti…………………………………………………………………....3
1.3 Umuhimu wa utafiti…………………………………………………………………4
1.4 Dhana ya istilahi,linux na nadharia ya uundaji
istilahi……………………………4
Sura ya pili:Mapitio ya marejeo na mbinu za ukusanyaji
data………………..8
2.1 Mapitio ya marejeo………………………………………………………………………….8
2.2 Mbinuza ukusanyaji data ……………………………………………………………..10
Sura ya tatu:Uchambuzi wa data………………………………………………11
3.1 Utangulizi………………………………………………………………………………….11
3.2 Mbinu zilizotumika katika uundaji wa istilahi za Kiswahili
katika Linux………….11
3.3 Ubora na udhaifu wa mbinu zilizotumika kuunda istilahi za
Kiswahili katka Linux…16
3.3.1 Ubora wa mbinu zilizotumika ……………………………………………………16
3.3.2 Udhaifu wa mbinu zilizotumika…………………………………………………18
3.3.3 Mbinu bora zaidi katika uundaji wa istilahi za
Kiswahili…………………………19
Sura ya nne:Muhtasari na Hitimisho…………………………………………..20
4.1 Matokeo ya utafiti kwa muhtasari…………………………………………………………20
4.2 Hitimisho…………………………………………………………………………………….22
Marejeo
Viambatisho
SURA YA KWANZA
1.0 Utangulizi
Lugha ni kielelezo cha maisha ya jamii kwani huenda sambamba na
mabadiliko au maendeleo katika jamii. Kila sekta ya jamii iwe
siasa,elimu,sayansi,teknolojia,utamaduni,dini,kilimo,uhandisi,sanaa,uchumi ama
biashara hubadilika kila mara .Uvumbuzi mpya kila mara huzua dhana mpya ambazo
zinahitaji maneno mapya kuzielezea(King’ei 2010)
King’ei(ameshatajwa) anaendelea kusema kuwa ukuzaji wa
msamiati na istilahi ni jambo la kawaida katika kurekebisha lugha ili iweze
kuambatana na wakati au iwe ya kisasa. King’ei anaendelea kusema kuwa ukuzaji
upya wa istilahi hufanyika kwa sababu mbalimbali.Kwanza kabisa lugha sharti
iweze kuelezea dhana mpya zinazoingia katika jamii kutokana na mabadiliko
katika jamii.Sababu ya pili ni kwamba maana ya maneno yanayotumika katika lugha
hupanuliwa ili kuchukua maana mpya au pana kuliko ile ya awali.Sababu ya tatu
ya kuwepo haja ya kustawisha istilahi mpya katika lugha ni ile haja ya kufasiri
maandishi kutoka lugha moja hadi nyingine.
Msanjila na wenzake (2011) wanasema hadi wakati huu lugha ya
Kiswahili imekwisha ingizwa katika mifumo miwili ya kompyuta ijulikanayo kama linuksi na mikrosofti.Wanaendelea
kusema,kuingizwa kwa Kiswahili katika mifumo hii maana yake ni kwamba mtumiaji
anaweza kuvinjari mifumo hiyo ya kompyuta kwa Kiswahili akiamua kufanya hivyo.
Pia King’ei(ameshatajwa) anaelezea kuwa,kampuni ya talakirishi
iitwayo microsoft ilitekeleza hatua ya kihistoria mwaka
2005 kwa kuanzisha kamusi maalumu inayo wawezesha watumiaji wa talakirishi
kutumia lugha ya Kiswahili katika mawasiliano yao yote kwa kompyuta,anaendelea
kusema,programu hii mpya inamwezesha mtumiaji kompyuta asiyefahamu lugha
nyingine kama vile kiingereza kutumia kompyuta na kuwasiliana bila shida
yoyote.
Katika mchakato wa kuziweka programu hizi katika Kiswahili,
ilihitajika kuunda istilahi za
Kiswahili ili kukamilisha shughuli hii mbinu mbalimbali za uundaji
istilahi zilitumika.
Katika uundaji wa istilahi za Kiswahili kuna mbinu mbalimbali
zinazotumika. Kwa mujibu wa
Kiango(2004) amebainisha mbinu za kuunda istilahi za Kiswahili
kuwa ni pamoja na:Kubuni,anasema,njia hii inaweza kutumika katika kukabili
mazigira ya aina mbili; kubuni msamiati ambao utataja mambo yaliyomo katika
jamii ambayo hayajapata msamiati wa Kiswahili. Pili ni kubuni msamiati ambao
utataja mambo kutoka nje ya jamii yenye msamiati wa kigeni, mbinu nyigine ni
kukopa; kukopa kwa kutohoa msamiati wa kigeni,kukopa kwa kutafsiri msamiati wa
kigeni na kukopa kwa kuingiza maneno ya kibantu na lahaja na njia nyingine ni
ya kufupisha maneno.
Kahigi (2004) anasema mbinu za kuunda istilahi ni pamoja na:
unyambulishaji; unyambulishaji ni kupachika viambishi undaji ili kuunda neno
lenye dhana na muafaka. Mfano, modification→ukumushaji. Mbinu nyigine ni
ukopaji; ukopaji ni kuchukua neno kutoka lugha chanzi na kulitohoa ili likubaliane
na taratibu za kisarufi za lugha pokezi. Mbinu zingine zilizoainishwa na Kahigi
ni: tafsiri mkopo;ni aina ya tafsiri kutoka lugha chanzi ambayo ni ya moja kwa
moja, mbinu nyigine ni uundaji wa maneno mapya, mbinu hii huhusisha uundaji wa
maneno mapya ambayo yalikuwa hayapo kwenye lugha lengwa, mfano byte
> baiti, uambatani; ni uwekaji wa maneno mawili au zaidi
yanayowakilisha dhana moja, mfano magneticfield >ugasumaku, ufupishaji; hii
ni mbinu ya kufinyanza maneno na kupata neno moja, mfano, UWT(Umoja wa Wanawake
Tanzania).
Mtafiti mwingine ambaye ameelezea mbinu za uundaji istilahi ni
Sewangi(2004) yeye anasema mbinu za uundaji istilahi ni pamoja na: kutohoa,kwa
mfano; computer > kompyuta, program>programu, mbinu nyingine ni kubuni,
kwa mujibu wa Sewangi anasema, mbinu ya kubuni inaweza kufanywa kidhahania au
kwa kutumia vigezo mahususi. Kubuni istilahi kidhahania
hutetewa kwa hoja kuwa hakuna uhusiano wa moja kwa moja baina ya istilahi na
dhana inayo bebwa, hivyo neno lolote laweza kuundwa na kupewa hadhi ya istilahi
ya dhana fulani. Njia mojawapo ya kuunda istilahi kidhahania ni kutumia fomula
za kompyuta ambapo maneno mengi yanaweza kuzalishwa na kupachikwa dhana
mahususi katika uwanja fulani wa maarifa. Njia ya kuunda istilahi kivigezo
huweza kufanywa kwa kutumia vigezo mahususi kama
vile kazi, umbo au mwonekano wa kitu. Kwa mfano kwa kutumia kigezo
cha kikazi kisawe cha calculator kimebuniwa kuwa ni kikokotozi (kitu
kinachofanya kazi ya kukokotoa), kisawe cha data saver kimekuwa kihifadhi data (kitu
kinachohifadhi data). Mbinu nyingine iliyoainishwa na Sewangi ni mbinu ya
kupanua maana ya maneno yaliyopo; njia hii huchukua neno lenye maana ya jumla
na kuliongezea maana ya kihistilahi katika mazingira ya kitaalamu, kwa mfano
neno kifaru ambalo maana yake ya jumla ni mnyama lakini katika mazingira ya
utaalamu wa kijeshi ni kisawe cha tank.
Kwa kuzingatia maelezo ya wataalamu hawa kuna mbinu tofautitofauti
za kuunda istilahi. Kwa hiyo kutokana na kwaba kuna mbinu tofautitofauti za
kuunda istilahi,utafiti huu hulenga kubainisha mbinu zilizotumika katika kuunda
istilahi za Kiswahili zilizoingizwa katika mfumo wa kompyuta wa linux.
1.1 Tatizo la utafiti
Kulingana na tafiti za wataalamu hawa,wameelezea kuingizwa kwa
Kiswahili katika mifumo ya kompyuta ya linux na Microsoft,kwa
mfano, Msanjila na wenzake (2011) na King’ei (2010) wameelezea kuhusu hili.
Vilevile wataalamu wengine kama vile Kiango (2004), Sewangi (2004) na Kahig
i(2004) wao wameainisha mbinu mbalimbali za kuunda istilahi za Kiswahili. Kwa ujumla
wataalamu hawa hawajaonyesha mbinu zilizotumika katika uundaji wa istilahi za
Kiswahili zilizoingizwa katika mifumo ya mawasiliano ya kompyuta hususani mfumo
wa kompyuta wa linux,kwa hiyo utafiti huu hulenga kuziba pengo hili
kwa kuchunguza mbinu zilizotumika katika uundaji wa istilahi za Kiswahili
katika linux.
1.2 Malengo ya utafiti
Malengo ya utafiti huu yamegawanyika katika sehemu kuu mbili:
1.2.1 Lengo kuu na
1.2.2 Malengo mahususi
1.2.1 Lengo kuu
Lengo kuu la utafiti huu ni kutaka kutalii istilahi za Kiswahili
zilizoingizwa katika mfumo wa mawasiliano ya kompyuta wa linux na
kuainisha mbinu zilizotumika kuunda istilahi hizo.
1.2.2 Malengo mahususi
Malengo mahususi ya utafiti huu ni mawili, ambayo ni: kupambanua
ubora na udhaifu wa mbinu zilizotumika katika uundaji wa istilahi za Kiswahili
katika linux na kubainisha mbinu bora zaidi inayoweza
kutumika katika uundaji wa istilahi za Kiswahili.
1.3 Umuhimu wa utafiti
Umuhimu wa utafiti huu ni kwamba utasaidia kubainisha mbinu bora
za uundaji wa istilahi za Kiswahili. Vilevile utafiti huu utawasaidia watumiaji
wa kompyuta wanaotumia programu hii ya linux kwa Kiswahili kuelewa kwa urahisi
istilahi zilizotumika baada ya kubainisha mbinu zilizotumika katika kuunda
istilahi hizo.
1.4 Dhana ya istilahi, linux na nadharia ya uundaji istilahi
Istilahi ni dhana
iliyofasiliwa na wataalamu mbalimbali na wote wanakubaliana kuwa, istilahi ni
msamiati utumikao katika uwanja fulani maalumu wa lugha. Wataalamu
wanaokubaliana na fasili hii ni pamoja na King’ei(2010), Samson(1988) na
Kiango(2004). Kwa hiyo kulingana na fasili hii si kila msamiati ni istilahi
bali msamiati huwa istilahi pale unapotumika katika Nyanja maalumu za kitaaluma.
Kila uwanja maalumu wa kitaaluma huwa na msamiati wake ambao hauna maana nje ya
taaluma hiyo wala haufahamiki kwa wazungumzaji lugha wasiokuwa wataalamu wa
lugha hiyo. Kwa mfano msamiti unaotumika katika isimu,fasihi,teknolojia ya
habari na mawasiliano na kadhalika ni maalumu na hutumiwa na kueleweka tu na
wataalamu wahusikao na nyaja husika.
Linux kwa mujibu wa
Msanjila na wenzake(2011) ni mfumo wa kompyuta huria unao ruhusu watu
mbalimbali kuchangia katika marekebisho na maendeleo yake. Kimsingi linux ni
mfumo endeshi wa kompyuta. Ni program katika kompyuta iayosaidia
programu-tumizi na mtumiaji wa kompyuta kufikia vifaa fulani katika kompyuta
ili kufanya kazi iliyokusudiwa, linux ni sawa na
program-tumizi zingine kama vile windows (Linux.com).
Nadharia ya uundaji istilahi hujumuisha mambo kadhaa, kwa mujibu wa Tumbo-Masabo na
Mwansoko(2008) mambo hayo ni pamoja na sababu za uundaji wa istilahi, njia au
mbinu za uundaji istilahi,vyombo vya uundaji istilahi na misingi ya uundaji
istilahi.
Katika sababu ya uundaji istilahi Tumbo-Masabo na Mwansoko
wanasema kuwa, uundji wa istilahi ni muhimu panapotokea haja ya kushughulikia
nyanja ambazo zilikuwa hazishughulikiwi kwa kutumia lugha fulani. Uundaji huo
aghalabu hufanywa ili kukidhi haja ya mawasiliano katika elimu ya juu, ufundi
na utaalamu,na shughuli zinazohusu serikali na teknolojia. Kwa hiyo nadharia ya
uundaji istilahi huambatana na sababu au haja fulani ya kufanya hivyo. Kwa
mfano uundaji wa istilahi za Kiswahili katika mfumo wa kompyuta wa linux umeambatana
na sababu kwamba, kuuweka mfumo huu wa kompyuta katika Kiswahili ili
kusudi watumiaji wa Kiswahili waweze kuutumia mfumo huu kwa lugha wanayo
ifahamu.
Vyombo vinavyohusika katika uundaji wa istilahi.
Katika kutekeleza kazi ya kuunda istilahi vimewekwa vyombo maalumu
vinavyo tekeleza suala hili, kwa mfano Tanzania chombo kilchopewa jukumu hili
na serikali ni Barza la Kiswahili la Taifa (BAKITA).
Vilevile katika nadharia ya misingi ya uundaji istilahi huzingatia
mambo yafuatayo:
· Uundaji wa istilahi ni budi uanzie kwenye dhana.
· Dhana hizo zieleweke kwa ukamilifu na uwazi.
· Uhusiano baina ya dhana ndio uwe msingi wa
uundaji wa istilahi, istilahi kopwa zichukuliwe kama zilivyo katika umbo lake
la asili kwa kufanya marekebisho machache tu kulingana na sarufi na matamshi ya
lugha kopaji.
· Istilahi inafaa ziwe fupi iwezekanavyo lakini
zieleweke.
· Istilahi ziwe na muundo unaoeleweka yaani
zifuate mofolojia ya lugha.
· Uundaji wa istilahi kwa vifupisho na akronomia
uepukwe hasa kama istilahi kamili si ndefu sana.
· Istilahi zisiwe na sinonimia au homonimia.
· Istilahi ziundwe kwa njia ambayo itakuwa rahisi
kuunda istilahi nyingine kwa
mnyambuliko.
· Istilahi zitolewe kufuatana na mfumo wa dhana
yaani ziainishwe kuliko kuandikwa kwa alfabeti.
· Muundo wa istilahi udokeze maana yake kwa
watumiaji wa lugha husika. Kwa hiyo misingi hii haina budi kufuatwa katika
mchakato wa uundaji istilahi.
Nadharia nyingine kama ilivyoainishwa na Tumbo-Masabo na
Mwansoko(wameshatajwa) ni njia za uundaji istilahi. Katika uundaji wa istilahi
kuna njia kuu mbili ambazo zinatumika zaidi, njia hizo ni pamoja na:
(i) Kutafsiri hasa kutoka kwenye lugha
zinazojulikana kuwa ni za kimataifa kama vile Kifaransa, Kiingereza,
Kihisipania.
(ii) Kuunda istilahi kutokana na mifumo ya dhana.
Njia ya kutafsiri hutumiwa sana na vyombo vingi vya uundaji
istilahi kinyume na misingi ya uundaji ambayo inasisitiza kuwa uundaji huo
uanze na dhana, msingi wa njia hii ni istilahi za lugha chasili ambazo aghalabu
hupangwa kwa alfabeti. Faida ya njia hii ni kwamba istilahi nyingi zinaweza
kushughulikiwa kwa muda mfupi pia istilahi za lugha lengwa huweza
kutafsiriwa katika lugha za kimataifa. Hata hivyo hasara ya njia hii ni kwamba
kwa vile kila istilahi hushughulikiwa peke yake, hali hii huweza kusababisha
mtiririko wa mfumo wa istilahi usio na ulingano.
Kahigi (2004) anasema kuunda istilahi kutokana na mifumo ya
kidhana ni kwamba istilahi huundwa kufuatana na mifumo hiyo. Kwa mfano katika
hisabati kuna mifumo ya elimu-maumbo, elimu-namba, vipimo na kadhalika.
Mathalani katika kuunda istilahi za dhana ya pembe itabidi dhana zifuatazo
zishughulikiwe zote kwa pamoja: pembekali, pembenukta, pembetatu,
pembemshabaha, pebemstari na kadhalika. Faida ya mkabala huu ni kwamba mwishowe
mifumo yote ya dhana huwa na mtiririko wenye ulingano.
Katika nadharia hii ya njia za uundaji istilahi mbinu mbalimbali
hutumika, mbinu hizo ni pamoja na:mwabatano; hii ninjia ya uundaji
istilahi kwa kuambatanisha maneno mawili au zaidi yaliyo
huru. Mfano ; mbwa kichaa.
Mnyambuliko;ni
uundaji wa neno jipya kwa kuambatisha viambishi kewenye mzizi au shina la neno.
Mfano;wekeza > uwekezaji.
Muungano; hii
mbinu ni sawa na mwambatano isipokuwa katika muungano maneno mawili au zaidi
huunganishwa ili kuunda neno moja, mfano;kiini+macho >
kiinimacho.
Kupanua maana ya maneno; huu ni mchakato ambapo neno lililopo kwenye lugha hupewa
maana pana zaidi ya maana yake ya awali. Mfano butu maana yake ya kawaida ni
–sio kali,-sio kata. Maana ya kihistilahi ni pembe ambayo ni zaidi ya nyuzi 90
na ndogo kuliko nhyuzi180(hisabati).
Ufupisaji; ni
mbinu ambayo inatumika kufinyanza fungu la maneno ili kuunda neno moja,mfano;
BAKITA (Baraza la Kiswahili laTaifa).
Ukopaji; ni matumizi ya neno
kutoka lahaja ama lugha nyingine, aghalabu neno hilo hubadilishwa ili lishabihi
muundo wa lugha lengwa.
Tafsiri-sisisi; ni aina ya tafsiri kutoka lugha chasili ambayo ni ya moja
kwa moja. Mfasiri habadili lolote ila anahakikisha tu tafsiri inakuwa sahihi
kwa mujibu wa lugha lengwa. Kwa hiyo katika mchakato wa uundaji wa istilahi za
Kiswahili mbinu hizi hutumika.
++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++
SURA YA PILI
Mapitio ya marejeo na mbinu za utafiti.
2.1 Mapitio ya Marejeo
Kutokana na mabadiliko yanayotokea katika jamii wataalamu
wameonesha umuhimu wa lugha kuyakabili mabadiliko hayo. King’ei(2010) anasema
lugha ni kielelezo cha maisha ya jamii siasa, elimu, sayansi, teknolojia,
utamaduni, dini, kilimo, uhandisi, sanaa, uchumi ama biashara hubadilika kila
mara, uvumbuzi mpya kila mara huzua dhana mpya ambazo zinahitaji maneno mapya
ya kuzielezea.
Kulingana na kukua kwa teknolojia ya habari na mawasiliano,lugha
ya Kiswahili haina budi kuyakabili mazingira haya. King’ei(ameshatajwa)
anaelezea hatua ya kihistoria iliyochukuliwa na kampuni ya Microsoft mwaka
2005 kwa kuanzisha kamusi maalumu inayowawezesha watumiaji wa kompyuta kutumia
lugha ya Kiswahili katika mawasiliano yao yote kwa kompyuta. Kwa maana kwamba
katika programu hii mpya inamwezesha mtumiaji kompyuta asiyefahamu lugha
nyingine kama vile kiingereza, kutumia kompyuta na kuwasiliana bila shida
yoyote kwa Kiswahili.
Mtafiti mwingine ni Msanjila na wenzake(2011) wanasema hadi wakati
huu lugha ya Kiswahili imekwisha ingizwa kwenye mifumo miwili ya kompyuta
ijulikanayo kama linuksi na mikrosofti.
Wanaendelea kusema kuingizwa kwa Kiswahili katika mifumo hii maana yake ni
kwamba mtumiaji anaweza kuvinjari mifumo hiyo ya kompyuta kwa Kiswahili akiamua
kufanya hivyo.
Kimsingi hatua ya kuingiza Kiswahili katika mifumo hii ya kompyuta
ni hatua muhimu sana katika maendeleo ya teknolojia ya habari na mawasiliano,
katika mchakato wa kuiweka mifumo hii katika lugha ya Kiswahili ilihitajika
kuundwa istilahi za Kiswahili ili mifumo hii iwekwe katika Kiswahili. Katika
kuunda istilahi za Kiswahili mbinu mbalimbali hutumika, wataamu mbalimbali
wamejadili kuhusu mbinu hizo:
Tumbo-Masabo na Mwansoko(2008) wanasema mbinu za uundaji istilahi
ni pamoja na: Muungano wa maneno, mfano; mwanaisimu, mwambatano
wa maneno, mfano; nusu kipenyo,
8
Unyambulishaji, mfano; ambisha > uambishaji, upanuzi wa
maana za maneno, uhulutishji, mfano; kizigeu >
kiziogeu, ukopaji (kukopa kutoka lugha za kigeni, lugha za
kibantu au lahaja) na tafsiri-sisisi (tafsiri mkopo), mfano;
measure of time > kipimo cha wakati.
King’ei(2010) ameainisha mbinu za uundaji wa istilahi za Kiswahili
kuwa ni pamoja na uunganishaji wa maneno, ukopaji, kutafsiri maneno ya
kigeni, mbinu ya ufupishaji mfano;UKIMWI (Upungufu wa Kinga Mwilini)
na utohozi.
Kahigi (2004) anasema mbinu za uundaji wa istilahi za Kiswahili ni
pamoja na:unyambulishi, uambatani, uhulutishi, ufupishaji, utemaji, ukopaji,
tafsiri mkopo na uundaji wa maneno mapya kabisa.
Vilevile Kiango (2004) ameanisha mbinu zifuatazo katika undaji wa
istilahi za Kiswahili: kubuni nakukopa (kutoka lugha za
kigeni, lugha za kibantu na lahaja).
Kwa hiyo kulingana na wataalamu hawa tunaweza kuanisha mbinu za
uundaji wa istilahi za Kiswahili kuwa ni:
· Unyambulishji
· Muungano wa maneno
· Mwambatano wa maneno
· Ukopaji
· Tafsiri mkopo(tafsiri sisisi)
· Uhulutishaji
· Ufipishaji
· Utemaji
· Upanuaji wa maana ya maneno yaliyopo na
· Kubuni
Tafiti za wataalamu hawa zina umuhimu mkubwa kwani zimesaidia
kujua kuingizwa kwa Kiswahili katika mifumo ya kompyuta ya linux na Microsoft na
vilevi zimetusaidia kujua mbinu za uundji istilahi za Kiswahili. Kwa hiyo
katika utafiti wetu tutabainisha mbinu zilizotumika
kuunda istilahi za Kiswahili katika linux kati ya
hizo zilizoainishwa na wataalamu hao
2.2 Mbinu za ukusanyaji data
Katika utafiti huu mbinu iliyotumika ni moja, yaani mbinu ya
kusoma marejeo mbalimbali hii ni kwa kuwa utafiti huu ni wa kimakitaba. Mbinu
hii imetumika katika ukusanyaji wa data zinazohusu istilahi za Kiswahili
zilizoingizwa katika mfumo wa kompyuta wa linux, ambapo mbinu
hii imetumika kwa kusoma marejeo kwa njia ya wavuti na kukusanya istilahi
za Kiswahili zilizokuwepo katika mfumo wa kompyuta wa linux.
Mbinu hii pia imetumika katika kukusanya data zinazohusu mbinu za
uundaji istilahi za Kiswahili. Kwa kusoma marejeo mbalimbali data zinazohusu
mbinu za uundaji wa istilahi za Kiswahili zilikusanywa.
Vilevile mbinu hii imetumika katika ukusanyaji wa data zinazohusu
ubora na udhaifu na udhaifu wa mbinu zilizotumika katika uundaji wa istilahi za
Kiswahili katika linux. Na pia mbinu hii imetumika katika
ukusanyaji wa data zinazohusu kubainisha mbinu bora katika kuunda istilahi za
Kiswahili.
Data katika utafiti huu
zimekusanywa kutoka faharasa ya teknolojia ya habari ya KILinux(KlnX)
juzuu ya kwanza. Faharasa hii inajumuisha orodha ya istilahi 700. Sampuli ya
utafiti huu inajumuishaistilahi 100. Sampuli hii imechukuliwa
kinasibu (kiholela) yaani hakuna mpangilo au utaratibu wowote maalumu uliofutwa
katika uchukuaji wa sampuli.
+++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++
SURA YA TATU
Uchambuzi wa data
2.1 Utangulizi
Utafiti huu umegawanyika katika sehemu kuu mbili, sehemu ya kwanza
inahusu uchambuzi wa data zinazohusu mbinu zilizotumika katika uundaji wa
istilahi za Kiswahili katika linux na sehemu ya pili
inahusu kupambanua ubora na udhaifu wa mbinu zilizotumika kuunda istilahi za
Kiswahili katika linuxna kubainisha mbinu iliyo bora katika kuunda
istilahi za Kiswahili. Katika uchambuzi wa data hizi tutatumia nadharia ya
uundaji istilahi za Kiswahili ambayo imekwishaongelewa katika kipengele cha
1.4.
2.2 Mbinu zilizotumika katika uundaji wa istilahi za
Kiswahili zilizoingizwa katika linux.
Mbinu zilizotumika katika uundaji wa istilahi za Kiswahili katika
linux ni kama zilivyobainishwa hapa chini:
Unyambulishi; katika
mbinu hii kitenzi kinaweza kugeuzwa kikawa nomino au kivumishi kinaweza
kugeuzwa kikawa kitenzi au au nomino. Mbinu hii imetumika kwa kiasi kikubwa,
mifano ifuatayo hudhihirisha matumizi ya mbinu hii.
· Accessing > ufikio (
viambishi u-i-o vimeambatiswa katika shina fika).
· Accsess
> fikio (viambishi i-o vimenyambulishwa katika
shina fika )
· Allocation
> utengaji (viambishi u-aji vimeambatishwa katika
shina tenga)
· Bookmark link >
alamisho (viambishi ish-o vimeambatishwa katika shina alama).
· Bookmark >
alamisha(t) (viambishi ish-a vimeambatishwa na kuunda kitezi alamisha)
· Deleting >
ufutaji (viambishi u-aji vimeambatishwa katika kitenzi futa )
· Deletion
> mfuto (viambishi m-o vimeambishwa katika kitenzi futa
nakupata
neno
mfuto)
· Input > ingizo
(kiambishi –o kimeambishwa katika shina ingiza na kuunda istilahi ingizo).
· Interactive >
wasilianifu ( kiambishi –ifu kimeambishwa katika shina wasiliana na kuunda neno
wasilianifu).
· Allocation(n) >
mtengo (viambishi m-o vimeambishwa katika shina tenga na kuunda nomino mtengo
ikiwa na dhana ya matokeo).
Mwabatano; hii
ni njia inayotumika kwa kuambatanisha maneno mawili au zaidi. Katika linux kuna
istilahi zenye mwambatano wa maneno mawili na mwambatano wa maneno matatu.
Mifano ifuatayo inadhihirisha matumizi ya mbinu hii:
· Add-on help > msaada
nyongeza ( yameambatishwa maneno msaada na nyongeza).
· Alphabet text character
> kiwambo alfabeti (kiwambo + alfabeti).
· Aperture value
> thamani upenyo (thamani + upenyo)
· Background colour
> rangi usuli (rangi + usuli).
· Block device
> kitunza data ( (ki)tunza + data).
· Bullet list >
orodha tobwe (orodha + tobwe).
· Composer
> programu tumizi (programu+ tumizi).
· Configuration utility
> programu sanidi (programu + sanidi).
· Checksum
> namba thibitishi (namba + thibitishi).
· Encrypted
> msimbo fiche (msimbo + fiche).
Vilevile kuna istilahi
zilizoundwa kwa kuambatanisha maneno matatu. Mfano:
· Encrypted text >
matini-msimbo fiche (matini + msimbo + fiche).
· Full-screen mode >
modi-skrini nzima (modi + skrini + nzima).
· Small caps
> herufi kubwa ndogo (herufi + kubwa + ndogo)
· Column spam >
upana-safu wima (upana + safu + wima).
· Default search engine
> injini tafuti-msingi (injini + tafuti + msingi).
· Com port (communication port) > mlango
wa mawasiliano(mlango+wa+mawasiliano).
Muungano; hii ni mbinu ya kuunganisha maneno mawili
au zaidi ili kupata neno moja mbinu hii pia imetumika kuunda istilahi za
Kiswahili katika linux. Mifano ifuatayo inabainisha
kutumika kwa mbinu hii:
· Anonymity >
ufichojina (uficho + jina).
· Arccosine >
kosinitao (kosini + tao).
· Backslashes >
mkwajunyuma ( mkwaju + nyuma).
· Data area
> eneodata (eneo + data).
· Data bank >
kanzidata (kanzi + data).
· Data base
> kihifadhidata ( (ki)hifadhi + data).
· Footnote
> tiniwayo (tini + wayo).
· Hypertext >
matinifora (matini + fora).
· Keybody >
baobonye (bao + bonye).
· Newsgroup >
kundihabari (kundi + habari).
· Spreadsheet >
lahajedwari (laha + jedwari).
Ukopaji; njia hii pia imetumika kuunda isuilahi za
Kiswahili katika linux. Mifano ifuatayo inaonyesha kutumika kwa mbinu hii.
· Account >
akaunti
· Adapter >
adapta
· Ampersand > ampasendi
· Applet >
apuleti
· Autoformat >
fomati otomati
· Baud
> baudi
· Boolean >
buleani
· Buffer
> bafa
· Cursor
> kasa
· Daemon > dimoni
· Dial
> dayo
· Digit > dijiti
· Icon >
ikon
· Kilobyte
> kilobaiti
· Pixels
> pisel
· Printer > printa
Mbinu hii ya ukopaji
imetumika kwa kiasi kikubwa katika uundaji wa istilahi za Kiswahili zilizopo
katika linux.
Mbinu nyingine
iliyotumika kwa kiasi kikubwa katika uundaji wa istilahi za Kiswahili katika
linux nimbinu ya tafsiri mkopo (tafsiri sisisi). Tafsiri mkopo
nitafsiri ya moja kwa moja kutoka lugha chanzi. Mifano ifuatayo inathibitisha
matumizi ya mbinu hii katika uundaji wa istilahi za Kiswahili katikalinux.
· Actions menu > menyu
vitendo.
· Address book > kitabu
cha anwani.
· Alert me
> nitahadharishe.
· Auto complete > kamilisha
kiotomati.
· Boolean operations
> matendo buleani.
· Certificate manager
> meneja ithibati.
· Certificate viewer
> kionyeshi hati.
· Chat group
> kundi sogozi.
· Colour capability
> uwezo kirangi.
· Connection failure
> unganisho shinde.
· Control panel
> paneli dhibiti.
· Country code
> msimbo nchi.
· Device manager
> meneja vifaa.
· Dialogue box
> kisanduku cha mawasiliano.
· Drag and drop >
kokota na dondosha.
· Eject
> fyatua.
· Flow control
> udhibiti wa mtiririko.
· Word processor
> kichakata matini.
· Web master
> mtawala tovuti.
Mbinu nyingine ni mbinu
ya kuunda maneno mapya kabisa mbinu hii imetawaliwa na maneno ya
mkopo. Mfano:
· Icon >
ikoni
· Italic >
italiki
· Label > lebo
· Megabyte(MB) >
megabaiti(MB)
· Menu proxies
> menyu proksi
· Manager >
meneja
· Pixels >
piseli
· Program >
programu
· Scan >
skani.
· Scanner > skana
· Tab >
tabo
· Tag > tagi
Mbinu ya ufupishaji pia imetumika katika kuunda istilahi za
Kiswahili katika linux; hii ni mbinu inayotumika kufinyanza fungu la maneno na
kupata neno moja. Mifano ifuatayo huonyesha matumizi ya mbinu hii:
· Alt(alternate)
> Kbdl (kibadala)
· BSS (Bulletin Board Service)
> HUM (Huduma za Ubao wa
Matngazo)
· Ctrl (ontrol)
> Kdbt (kidhibiti)
· ESC (escape) >
Epa (epuka)
· FAQ (frequently asked quetions)
> MYM (Maswali Yaulizwayo Mara kwa mara)
· FTP (file transfer protocol)
> IKF (Itifaki ya Kuhawalisha Faili)
· FYI (For Your Information)
> KTY (Kwa Taarifa Yako)
· Megabyte
(MB) >
megabaiti (MB)
· Ref:
> Yah:
· Re:
> Jb:
· TCP (Transfer Control
Protocol) > IKU
(Itifaki ya Kudhibiti Urushaji)
· URL (Uniform Resource Location)
> KISARA (Kioneshi Sanifu Rasilimali)
· WWW (World Wide
Web) > WWW (Wavu Wa
Walimwengu)
Uhulutishi ni mbinu pia liyotumika katika uundaji wa
istilahi za Kiswahili katika linux, mbinu hii hutumika katika
uundaji wa istilahi kwa kuunganisha sehemu za maneno na kuunda neno moja. Mbinu
hii imetumika kwa kiasi kidogo sana, rejea mifano ifuatayo:
· Bitmap >
taswidoti ( (taswi)ra + doti)
· Multimedia >
medianuwai ((medi)a + anuwai)
Mbinu nyingine
iliyotumika katika uundaji wa istilahi za kiswahili katika linux lakini
kwa kiasi kidogo sana ni ile mbinu ya upanuzi wa maana za maneno,
upanuzi wa maana za maneno ni kuongezea maana maalumu za kihistilahi katika
maneno ya Kiswahili. Mfano:
· Mouse
> puku
Puku kwa maana ya
kawaida ni panya pori lakini hapa limepewa dhana mahususi katika kompyuta kwa
maana ya kifaa kinachotumika katika utumiaji wa kompyuta.
Utemaji (clipping) ni mbinu pia iliyojitokeza kwa
kiasi kidogo sana, kwa kutumia mbinu hii istilahi huundwa kwa kukata sehemu ya
neno na sehemu ya neno itakayobaki hutumika kama istilahi. Mfano: key (on
keyboard) > kibonye ( kutoka neno
bonyeza na kuongeza kiambishi cha ngeli ya saba ki-).
Kwa hiyo hizi ndizo
mbinu zilizobainika kutumika katika uundaji wa istilahi za Kiswahili
zilizoingizwa katika mfumo wa kompyuta wa linux.
2.3 Ubora na udhaifu wa mbinu zilizotumika kuunda istilahi za
Kiswahili katika linux.
2.3.1 Ubora wa
mbinu zilizotumika.
Kwa kiwango kikubwa mbinu zilizotumika zimezingatia misingi na
kanuni za uundaji istilahi. Kwa mujibu wa Tumbo-Masabo na Mwansoko (2008)
wanabainisha kuwa misingi mahususi
katika uundaji wa istilahi ni pamoja na: Uangavu wa wa istilahi
iliyoundwa yaani istilahi ziakisi sifa bainifu za dhana zinazoziwakilisha.
Mbinu zilizotumika katika uundaji wa istilahi za Kiswahili katika linux kwa
kiasi kikubwa zimezingatia msingi huu. Kwa mfano:
Ufikio >
accessing, ingizo
> input,
alamisha > bookmark.
Istilahi hizi zinaonyesha wazi dhana zinazowakilishwa, kwa mfano,
alamisha inabeba dhana ya kitendo cha kuweka alama hivyo kwa msingi
huu inadhihirisha mbinu zilzotumika ni bora. Vilevile mbinu zilizotumika
zimezingatia msingi wa uundaji istilahi unaosema, istilahi sharti ziwe na uwezo
mkubwa wa kunyambuliwa na kuunda istilahi nyingine za kikoa au ukanda
unaohusika. Msingi huu umefuatwa katika kuunda istilahi za kwenye linux,
kwani istilahi nyingi zilizoundwa zina uwezo wa kunyambulishwa. Mfano:
· Add > ongeza
· Add-on >
nyongeza
· Alert(n)
> thadhari
· Alert(v)
> tahadharisha
Pia uundaji wa istilahi za kwenye linux umezingatia
msingi wa uundaji istilahi unaosema,uwakilishi wa istilahi moja kwa dhana moja.
Msingi huu umezingatiwa kwa kiasi kikubwa kwani istilahi takribani zote
huwakilisha dhana moja isipokuwa zile zilizoundwa kwa kupanua maana ambazo ni
chache sana.
Mfano: configuration > usanidi
Configuration file > faili sanidi
Vilevile mbinu zilizotumika ni bora kwani hazijatumia kwa kiasi
kikubwa mbinu za uhulutishi na mbinu ya kupanua maana ya maneno yaliyopo, hii
ni kwa sababu misingi ya uundaji wa istilahi za Kiswahili husisitiza kuepuka
matumizi ya mbinu hizi; hii ni kwa kuwa istilahi zinazo uundwa kwa mbinu ya
uhulutishi huwa na uvulivuli wa maana na kufanya kuwa ngumu kukumbukwa na
kutumiwa. Pia uundaji wa istilahi kwa kupanua maana ya maneno yaliyopo
husababisha watumiaji wa istilahi hizi kushindwa kutofautisha maana zake za
kawaida na zile za
kihistilahi.
Mbinu za uundaji istilahi za Kiswahili katika linux, pia
zimezingatia msingi wa uundaji wa istilahi za Kiswahili unaosema, istilahi
sharti ziwe fupi na zenye kueleweka. Istilahi nyingi zimeundwa kwa kuzingatia
msingi huu.
2.3.2 Udhaifu wa mbinu zilizotumika
Katika uundaji wa istilahi za Kiswahili za kwenye linux, kuna
baadhi ya mbinu zilizotumika zinazoonyesha kuvunja kanuni na misingi ya uundaji
istilahi. Kwa mfano kuna istilahi zilizoundwa kwa kukiuka msingi wa uundaji
istilahi unaosema, istilahi sharti ziwe fupi na zenye kueleweka. Kuna baadhi ya
istilahi ambazo ni ndefu na hivyo kukiuka huu msingi. Mfano:
· Allow popup from this site
> ruhusu udukizi kutoka tovuti hii
· Com port
> mlango wa mawasiliano
Istilahi hizi zimeonekana kuwa ndefu kwa sababu mbinu iliyotumika
ni ya mwambatano wa maneno, na kwa mujibu wa Tumbo-Masabo na Mwansoko wanasema,
“iwapo istilahi zitaundwa kwa kutumia mbinu za muungano na mwambatano wa maneno
basi mambo yafuatayo itabidi yazingatiwe”:
i. Idadi ya maneno yanayounganishwa au
yanayoambatanishwa yafaa yasizidi mawili.
ii. Vistari visitumike kutenga istilahi ambatani
kwani katika Kiswahili istilahi za namna hii hutamkwa kama neno moja lenye
mkazo mkuu kwenye silabi moja tu.
iii. Istilahi za namna hii yafaa zisiwe na silabi
zaidi ya nane kwani kwa kawaida maneno ya Kiswahili yanawastani kati ya silabi
moja na tano tu. Kwa msingi huu mifano ya itilahi zilizotolewa hapo juu
zimeundwa na maneno zaidi ya mawili na silabi zaidi ya nane. Mfano ; mlango wa
mawasiliano (silabi 10), ruhusu udukizi kutoka tovuti hii (silabi 15) na hivyo
huu ni udhaifu uliojitokeza.
Vilevile matumizi ya mbinu za uhulutishi na upanuzi wa maana ya
maneno yaliyopo zimetumika, huu ni udhaifu kwani misingi ya uundaji wa istilahi
za Kiswahili inasema, mbinu ya
uhulutishaji iepukwe kwani etimolojia yake ina uvulivuli na
uundaji wa istilahi kwa kupanua maana ya maneno yaliyopo yafaa uepukwe kwani
istilahi za namna hii zinawakanganya wengi hasa zinapotumika nje ya muktadha au
kwenye taaluma zenye mahusiano ya karibu.
Mifano ya istilahi zilizoundwa kwa uhulutishaji ni:
· Taswidoti
> bitmap
· Medianuwai
> multimedia
Na mfano wa istilahi iliyoundwa kwa upanuzi wa maana ya neno ni:
Puku > mouse. Puku ni
istilahi iliyopanuliwa maana ambapo maana yake ya kawaida ni panya pori lakini
maana yake maalumu ni kifaa kinachotumika katika utumiaji wa kompyuta.
Kwa hiyo huu ndio udhaifu wa istilahi zilizotumika katika uundaji
wa istilahi za Kiswahili katika linux.
2.3.3 Mbinu bora zaidi katika uundaji wa istilahi za Kiswahili.
Kulingana na utafiti huu mbinu zilizoonekana kuwa bora zaidi na
ambazo zinatumika sana katika uundaji wa istilahi za Kiswahili ni pamoja na,
unyambulishaji, ukopaji, mwambatano, muunganiko pamoja na tafsiri mkopo. Mbinu
hizi zimeonekana kuwa bora katika uundaji wa istilahi za Kiswahili kwa sababu
zinaruhusu uundaji istilahi kwa wingi iwezekanavyo na mbinu hizi huzingatia
misingi ya uundaji istilahi za Kiswahili. Misingi hiyo ni pamoja na ufaavu wa
kiisimu, uwekevu wa kiisimu, unyambulifu , uwakilishi wa istilahi moja kwa
dhana moja, udhahiri na utoshelevu pamoja na uangavu. Mbinu hizi huakisi kwa
kiasi kikubwa misingi hii na hivyo kupendekezwa na waunda istilahi katika uundaji
wa istilahi za Kiswahili.
SURA YA NNE
Muhtasri na Hitimisho
4.1 Matokeo ya utafiti kwa muhtasari
Utafiti huu umeongelea malengo matatu. Kwanza utafiti huu
umebainisha mbinu za uundaji istilahi zilizotumika katika linux. Pili utafiti
umepambanua ubora na udhaifu wa mbinu za uundaji istilahi za Kiswahili
zilizotumika katika linux. Tatu umebainisha mbinu bora zaidi katika uundaji wa
istilahi za Kiswahili.
Utafiti huu umeonyesha kuwa mbinu kumi za uundaji istilahi za
Kiswahili zimetumika katika istilahi za linux. Mbinu hizo ni pamoja na:
Unyambulishi; mifano
ya istilahi zilizoundwa kwa mbinu hii ni kama vile:
· Ufikio >
accessing
· Utengaji > allocation
· Alamisho >
bookmark link
· Ingizo > input
Muungano wa maneno; mifano ya istilahi zilizoundwa kwa mbinu hii ni pamoja na:
· Ufichojina > anonymity
· Mkwajunyuma >
backslashes
· Kanzidata
> databank
Ukopaji; mbinu hii pia
imetumika katika kuunda istilahi za kwenye linux. Mfano:
· Akaunti >
account
· Apuleti
> applet
· Dayo >
dial
Tafsiri mkopo (tafsiri sisisi); mifano ya istilahi zilizoundwa kwa kutumia mbinu hii ni:
· Menyu vitendo
> actions menu
· Meneja ithibati
> certificate manager
· Paneli dhibiti
> control panel
Mwambatano;
mbinu hii vilevile imebainishwa kutumika katka uundaji wa istilahi za Kiswahili
katika linux:
Mifano: Rangi usuli
> background color
Orodha tobwe > bullet list
Thamani upenyo > aperture value
Kuunda maneno mapya kabisa; mbinu hii pia imetumika. Mfano.
· Ikoni > icon
· Italiki >
italic
· Menyu proksi > menu
proxies
Ufupishaji; katika
utafiti huu mbinu hii pia imetumika. Mfano:
· Kbdl (kibadala) > Alt
(alternative)
· Kdbt (kidhibiti)
> Ctrl (control)
· Epa (epuka)
> Esc (escape)
· KISARA (Kioneshi Sanifu Rasilimali )
> URL (Uniform Resource Location)
Uhulutishi; mbinu hii pia imetumika. Mfano:
· Taswidoti > bitmap
· Medianuwai >
multimedia
Upanuzi wa maana; mfano, puku (panya pori) > mouse.
Utemaji (clipping); mbinu hii pia imetumika. Mfano, kibonye
> key (on keybody).
Kwahiyo hizi ndizo jumla ya mbinu zilizo tumika kuunda istilahi za
Kiswahili katika linux.
Matokeo ya utafiti huu yanaonyesha mbinu zilizotumika ni bora kwa
kiasi kikubwa hii ni kutokana na sababu kwamba, mbinu zilizotumika zimezingatia
misingi na kanuni za uundaji istilahi kwa kiasi kikubwa. Lakini vilevile baadhi
ya mbinu za uundaji istilahi zimetumika
ambazo kwa mujibu wa misingi ya uundaji istilahi hazifai kutumiwa
katika mchakato wa uundaji wa istilahi za Kiswahili. Mbinu hizi ni pamoja na
uhulutishi na upanuzi wa maana ya maneno yaliyopo.
Pia utafiti huu umebainisha mbinu bora katika uundaji wa istilahi
za Kiswahili kuwa niunyambulishaji, muungano wa maneno, uambatishi, mkopo
pamoja na tafsiri mkopo. Hii ni kwa sababu mbinu hizi huzingatia
misingi ya uundaji wa istilahi za Kiswahili kwa kiwango kikubwa.
3.2 Hitimisho
Katika mchakato wa uundaji wa istilahi za Kiswahili kuna misingi
ambayo hainabudi kufuatwa. Ili kuunda istilahi zilizobora mwanahistilahi
hanabudi kuzingatia misingi hii.
Kwa mujibu wa Tumbo-Masabo na Mwansoko (2008) wanasema kuwa ili
kuinua ubora wa istilahi za Kiswahili waundaji istilahi wanasisitizwa
kuzingatia mambo matatu muhimu. Kwanza wanasisitizwa kwa kadri iwezekanavyo
wafuate kwa makini kanuni na taratibu za uundaji istilahi za Kiswahili. Kwa
kufanya hivi itawezesha kwa kiwango kikubwa kuundwa istilahi za Kiswahili zenye
kulandana vizuri kisarufi.
Pili waundaji istilahi wanahimizwa kuachana na mtindo wa kuunda
istilahi moja moja kukidhi mahitaji yao ya istilahi ya papo kwa papo kwani
mtindo huu unasababisha uundaji wa istilahi zisizo na mtiririko na
utimilifu wa kuridhisha. Kwa kuwa dhana zinazo wakilishwa na istilahi kwa
kawaida huwa hazikai pweke pweke bali hukaa kama seti au mifumo maalumu, basi
ni vema uundaji istilahi ufuate vilevile mifumo hiyo ya kidhana. Kulingana na
maelezo haya kinachosisitizwa ni uundaji wa istilahi kwa kuzingatia mifumo ya
kidhana. Kwa mujibu wa Tumbo-Masabo na Mwansoko (wameshatajwa) wakimnukuu Mkude
(1989:34) wanasema,
uundaji wa istilahi kwa kuzingatia mfumo wa kidhana unafaida kuu
nne:
(i) Utawasaidia waunda istilahi kuonyesha wazi
mantiki ya uhusiano baina ya istilahi za ukanda mmoja.
(ii) Utawahimiza waunda istilahi kubainisha vizuri
zaidi tofauti ndogondogo lakini muhimu baina ya istilahi zinazokaribiana.
(iii) Utawasaidia kutambua haraka mapengo katika
nasaba au upungufu katika maelezo.
(iv) Utawasaidia waunda istilahi kuona haraka ni
istilahi zipi zitaweza kuathiriwa upesi iwapo kutatokea mabadiliko katika
istilahi moja wapo.
Hivyo utaratibu wa uundaji istilahi kinasaba ukitumiwa utaepusha
uundaji wa istilahi zinazogongana na zisizo na mtiririko wenye mantiki.
Jambo la tatu kama ilvyoainishwa na Tumbo-Masabo na Mwansoko ni
kwamba uundaji wa istilahi haunabudi kuzingatia tofauti za watumiaji, mathalani
viwango vyao vya elimu, mazingira yao na kadhalika. Kwa hali hii ili
kuhakikisha istilahi bora za Kiswahili zinaundwa ni muhimu hadhira mahususi za
watumiaji istilahi ziainishwe na istilahi ziundwe kufuatana na viwango vya
elimu ya watumiaji lengwa. Ni kwa kufanya hivyo dhana kama vile istilahi angavu
au istilahi zenye uvulivuli zitakuwa na maana halisi kwani zitahusishwa na
vikundi mahususi vya watumiaji istilahi.
Na Aritamba Malagira.
Haki zote zimehifadhiwa.
MAREJEO
Kahigi,K.K (2004).Ujanibishaji wa office na windows xp kwa
Kiswahili sanifu katika
http//ajol.info.
Kiango,J.G (2004). Uundaji wa msamiti mpya katika
Kiswahili: Zoezi lenye njia mbalimbali
katika Kiango.htm.
King’ei, K (2010). Misingi ya isimujamii. Dar es
salaam. Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili.
Msanjila,Y.P, Kihore,Y.M na D.P.B Massamba (2011). Isimujamii
sekondari na vyuo.
Dar es salaam. Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili.
Samson, H.R (1988). Ufundi wa magari, mfano wa ukuzaji wa
istilahi za Kiswahili katika
Mulika na.21. Dar es salaam. Taasisi ya uchunguzi wa Kiswahili.
Sewangi,S.S (2004). Maana katika uundaji wa istilahi katika Sewangi,pdf.
Tumb-Masabo,Z.N.Z na Mwansoko,H.J.M (2008). Kiongozi cha
uundaji istilahi za Kiswahili.
Dar es salaam. Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili.
+++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++
SHAABAN
ROBERT KAMA MWANANATHARI
1.0.HISTORIA
FUPI YA MWANDISHI
1.1 UZAWA NA MAISHA YAKE
1.1.1 UPANDE WA BABA YAKE
Asili ya wazazi wa
Shaaban Robert ni Tunduru-Ruvuma kwa upande wa baba yake na Tanga kwa upande wa
Mama yake.
Babu yake Shaaban
Robert kwa upande wa baba aliitwa Kanduru. Alikuwa mzaliwa wa Wilaya ta
Tunduru, mkoani Ruvuma. Katika suala la imani ya Kidini, Kanduru alikuwa
anaamini Miungu ya Ki-mizimu ambayo wakati huo iliaminika kuwa ndiyo chanzo cha
yote yaliyojiri katika maisha ya binadamu. Kanduru alipofika Mzizima kwa mara
ya pili ili aje kufanya kazi, alimpata mke kutoka kabila la Wazaramo. Mke huyu
alikuwa Muislamu kwa sababu eneo lote la Pwani lilikuwa tayari linakaliwa na
wakazi wengi waliokuwa Waislamu. Kutokana na kumhitaji binti huyu, ilimlazimu
Kanduru asilimu kwanza ndipo aozwe. Hivyo, Kanduru alisilimishwa na kuwa
Mwislamu, akaitwa Jumaa, ndipo akaozwa.
Baada ya muda, walipata
mtoto waliyempa jina la Ufukwe, jina alilopewa na watani kwa kuwa alizaliwa
ufukweni mwa bahari ya Hindi wakati mama yake alipokwenda huko kutandaza Uduvi.
Pia aliitwa Selemani, jina ambalo lilikuwa rasmi kwa muktadha wa dini ya
Kiislamu. Tajiri wa Jumaa ambaye alikuwa mzungu, aliamua kumpa mtoto huyu jina
la Roberto kutokana na mapenzi na furaha aliyokuwa nayo. Hivyo jina hili
halihusiani na dhana ya dini. Baabaye, kutokana na athari za matamshi ya lugha
ya Kiingereza, jina hili la Roberto lilibadilishwa na kutamkwa Roberts. Roberto
au Roberts, ambaye majina yake ya Ufukwe na Selemani yalififia, alimuoa
Mwanamwema binti Mwindau na kuishi naye huko Vibambani, Tanga. Mnamo tare 01
Januari 1909, wakamzaa mtoto waliyemuita Shaaban.( Ponera 2010:26).
1.1.2 UPANDE WA MAMA YAKE
Bibi Mwanamwema binti
Mwidau alikuwa ni wa ukoo wa kina Kihere (yaani Kihere Mwalimu Kihere na
Mwalimu Mwalimu Kihere), ambao wanatajwa sana katika barua nyingi za Shaaban
Robert (kama zilivyo limbikizwa na kuhaririwa na M. M. Mlokozi). Alikuwa ni
wakabila la Kimwamwande, na alizaliwa Msengenyeni, Tanga, mwaka wa kuzaliwa
haujulikani. Alifariki mwaka 1967.
Bibi Mwanamwema
aliolewa mara tatu na alijaliwa kupata jumla ya watoto 14. Mume wake wa kwanza
alikuwa Bwana Kibwana. Huyu alizaa naye watoto 3, wa kiume wawili na mmoja wa
kike. Watoto hao ni:
(i)
Jafari Kibwana
(ii)
Mwanagani Kibwana (mwanamke)
(iii)
Khatib Kibwana
Kipindi cha kabla ya
Vita Vikuu vya Kwanza vya Dunia (1914-1918). Bwana Kibwana alisafiri kwenda
Uganda na hakurudi. Hivyo Bibie Mwanamwema akajikuta hana mume, na ndipo
alipoolewa na Bwana Selemani au Ufukwe bin Jumaa, au jina jingine Robert. Huyu
alikuwa ni Myao Upande wa baba, na Mzaramo upande wa mama, na alipewa jina la
“Robert” kwa heshima ya mkulima wa Kizungu ambaye baba yake, yaani Mzee Jumaa,
alikuwa akifanyia kazi.
Mwanamwema alizaa na
Bwana Ufukwe mtoto mmoja tu, yaani Shaaban Robert. Baadaye wakaachana. Hata
hivyo, Bwana Robert alikuwa na watoto wengine kwa wake wengine, ambao ni:
(i)
Jumaa bin Robert wa Ngamiani, Tanga
(ii)
Abdallah bin Robert wa Mnyanjani, Tanga
(iii)
Mwansaumu binti Robert wa Mnyanjani
Mume wa tatu wa Bibie
Mwanamwema alikuwa ni Bwana Mwinyiulenge Mworogo. Huyu alizaa naye watoto
10-wasichana watano na wavulana watano-wafuatao:
(i)
Mwishehe Ulenge (Mvulana)
(ii)
Mwanaidi Ulenge (msichana)
(iii)
Mwanang’andu Ulenge (msichana)
(iv)
Yusufu Ulenge (Mvulana)
(v)
Mwanahadia Ulenge (Msichana)
(vi)
Asha Ulenge (msichana)
(vii)
Mwidau Ulenge (msichana)
(viii)
Issa Ulenge (mvulana)
(ix)
Ali Ulenge (mvulana)
(x)
Maimuna Ulenge (msichana) (mulokozi:
2002:3)
1.1.3
SHAABAN ROBERT
Shaaban Robert
alizaliwa tarehe 01 Januari 1909, (Wakati wa ujana wake Shaaban aliacha
kuliandika jina la Roberts, akaanza kujiita Shaaban Robert), alipelekwa
madrasa, shule itoayo mafunzo ya dini ya Uislamu na mama yake akiwa na umri wa
miaka tisa. Huko alijifunza mambo mengi yahusuyo dini ya Uislamu kama vile
Hadithi za Mtume Mohammad (ambaye ni Kiongozi wa Waislam). Alianza masomo ya
elimu ya msingi mwaka 1922 katika shule ya msingi ya Kichwele (sasa inaitwa
Uhuru mchanganyiko) iliyopo mjini Dar es Salaam akiwa na umri wa miaka 13.
Wakati huo, tayari alikuwa amekwishapata elimu ya dini kwa kiwango kikubwa.
Aliendelea kusoma elimu hiyo ya dini hata alipokuwa anaendelea na masomo haya
ya shule ya msingi. Alihitimu masomo hayo mwaka 1926 na kufaulu vizuri kwa
kushika nafasi ya pili kati ya wanafunzi kumi na mmoja. Baada ya hapo,
aliajiriwa na serikali ya kikoloni na kufanikiwa kushika nyadhifa mbalimbali.
(Ponera 2010: 27).
1.2 KAZI ALIZOZIFANYA
·
Alianza na kazi ya Ukarani wa serikali
Forodhani Pangani mwaka 1926-1944.
·
Idara ya hifadhi ya Wanyamapori
(Mpwapwa) mwaka 1944-1946.
·
Alifanya kazi katika Afisi ya Mkuu wa
Jimbo Tanga mwaka 1946-1952.
·
Afisa wa kupima nchi Tanga (Idara ya
ardhi) mwaka 1952-1960.
·
Pia kabla hajastaafu mwaka 1960, aliwahi
pia kuhamishiwa Old Moshi.
Alipokuwa kazini
aliheshimika katika sehemu zote alizofanya kazi kutokana na adabu, bidii na
uadilifu wake.
1.3 KIFO CHAKE
Shaaban Robert
alifariki tarehe 20/06/1962 katika hospitali ya Mkwakwani Tanga, Bombo na
kuzikwa tarehe 22/06/1962 katika makaburi ya ukoo wa mama yake yaliyopo hapo
hapo Vibambani Tanga. Alifariki akiwa na miaka Hamsini na tatu (53).
Chanzo cha kifo chake
kinatajwa kuwa ni kufanya kazi kwa muda mrefu bila kupumzika. Pia wengine
wanataja kuwa ni kwa sababu ya homa ya Kifua Kikuu. Alilazwa katik hospitali
hiyo kwa muda mrefu akianzia katika wodi ya Kawaida kisha alihamishiwa katika
wodi ya wagonjwa mahututi. (Ponera 2010:29).
1.4 MAISHA YA NDOA
Mke wa kwanza wa
Shaaban Robert alikuwa ni Amina. Alimuoa mwaka 1930/1931. Aliishi naye kwa
miaka kumi tu ambapo walizaa watoto wengi lakini wengi walifariki wakiwa bado
wachanga.
Amina anakadiriwa
kufariki mwaka 1942 (Kutokana na shairi la Amina, kutungwa Juni 1942) na
kumwachia watoto wawili, ambao ni Selemani na Mwanjaa ambao walipona dhidi ya
mauti ya mapema. Kutokana na ubovu wa barabara na hali mbaya ya hewa,
alishindwa kusafirisha mwili wa Amina hadi Vibambani hivyo alimzika huko huko
Pangani.
Baada ya kufariki Amina
shaaban alitunga tenzi za Adili na Hatia kwa ajili ya Wanawe, Mwanjaa na
Selemani ili zisimame pahala pa marehemu mama yao kimalezi.
Shaaban Robert alikaa
takriban miaka mitatu bila ya mke hadi tarehe 14/09/1945 alipomwoa Bi Sharifa
binti Hussein wa Chumbageni Tanga, ambapo pia walizaa watoto wengi ambao pia
walifariki wakiwa wachanga ambapo watoto wanne tu walipona ambao ni Akili,
Hussein, Mwema na Ikibali.
Baadaye Ugane ulimvaa
tena Shaaban Robert, ambapo mke huyu wa pili alifariki mwaka 1955. Baada ya
kifo cha mke wake wa pili alioa mke wa tatu ambaye ni Bi. Mwanambazi binti Ali.
Huyu hakuzaa naye na ndiye aliyemkalia eda mara tu baada ya kifo chake tarehe
20/06/1962.
1.5 MWONEKANO WAKE WA JUMLA
Shaaban Robert alikuwa
ni Mcha Mungu ambapo alikuwa Mwislamu aliyeyazingatia maamrisho na miongozo ya
dini hiyo kama vile kusali sala tano na mengineyo.
Pia Shaaban Robert
alipenda kufurahi nakushirikiana na watu katika kazi na shughuli mbalimbali za
kijamii. Aliutumia muda wake mwingi kufanya kazi alizopanga na baada ya kazi alijikita
katika kuandika.
2.0 KAZI ZA KIFASIHI ZA SHAABAN ROBERT
Shaaban Robert ni
miongoni mwa waandishi maarufu na wakongwe wa fasihi ya Kiswahili ambao
wamejizolea umaarufu mkubwa kutokana na kuandika kazi mbalimbali za kifasihi
zenye kutumia ufundi na unadhifu mkubwa wa lugha ya Kiswahili. Miongoni mwa
waandishi hao ni kama vile Amri Abeid Kaluta, Mathias Mnyampala, Ibrahim
Hussein, Mohammed Said Abdulla, Penina Mhando na wengine wengi.
Shaaban Robert
amejipatia sifa kubwa ikilinganishwa na waandishi wengine kwani ana sifa za
kipekee/ upekee mkubwa unajitokeza katika vigezo vifuatavyo;
i.
Idadi ya kazi zake za kifasihi ni nyingi
ikilinganishwa na waandishi wengine.
ii.
Udhati, uendelevu na uhalisi wa maudhui
ya kazi zake.
iii.
Umaridadi wa ufundi wa uandishi wake.
Shaaban Robert ndiye
mwandishi pekee aliyeandika na kuchapisha kazi nyingi zaidi za kifasihi ya
Kiswahili kwa lugha ya Kiswahili (kazi zilizokwisha kuchapishwa mpaka sasa ni
ishirini na nne 24).
Aliandika kazi zilizo
katika makundi mawili ambayo ni Nudhumu na Nathari.
Kazi yake ya mwanzo
kabisa kuchapishwa ni makala ya “Hirizi ya shilingi mia” ambayo ilitoka katika
gazeti la Mambo Leo mwaka 1932. Baada ya hapo aliendelea kuandika kazi nyingi
za ushairi na nathari katika Magazeti.
Kisha alitunga tawasifu
yake “Maisha Yangu” (ambayo baadaye aliipanua na kuiita “Maisha Yangu na Baada
ya Miaka Hamsini”).
Mwaka 1939 ilianza Vita
vya Pili vya Dunia na kwisha 1945 wakati wote huo alitunga “Utenzi wa Vita vya
Uhuru” wenye beti 3000. Baada ya utenzi huo alianza kutunga nathari kama vile
Kufikirika, Kusadikika, Adili na Nduguze na kadhalika.
Hakuwahi kuandika kazi
yoyote ya Tamthiliya (Ponera 2010).
1
KAZI ZAKE ZA NUDHUMU NI;
1.
Masomo Yenye Adili, (1959), Art &
Lit, Nairobi.
2.
Utenzi wa Vita vya Uhuru (1961), Oxford,
Nairobi.
3.
Kielezo cha Fasili, (1962), Nelson,
Nairobi.
4.
Pambo la Lugha, (1966), Oxford, Nairobi.
5.
Insha na Mashairi, (1967), Nelson,
Nairobi.
6.
Ashiki Kitabu Hiki, (1968), Nelson,
Nairobi.
7.
Mapenzi Bora (1969) Nelson, Nairobi.
8.
Mwafrika Aimba, (1969), Nelson, Nairobi.
9.
Koja la Lugha, (1969), Oxford, Nairobi.
10.
Maisha ya Shaaban Robert, (1971),
Nelson, Nairobi.
11.
Sanaa ya Ushairi, (1972), Nelson, Nairobi.
12.
Almasi za Afrika, (1972), Nelson,
Nairobi.
13.
Tenzi za Maadili Mema na Omar Khayyam
(1973), T PH, Dar es Salaam.
13. 14. 2.2 KAZI ZAKE ZA NATHARI
Kazi za nathari za
Shaaban Robet zinajumuisha kazi za makundi yafuatayo;
(i)
Barua.
(ii)
Insha.
(iii)
Hadithi Fupi.
(iv)
Riwaya za Kiwasifu.
(v)
Riwaya za Kitawasifu.
Sifa
zilizotumika katika kutofautisha makundi haya (hususani hadithi fupi na Riwaya ni;
(i)
Urefu (idadi ya maneno).
(ii)
Uchangamano wa vitushi (sahili na tata).
(iii)
Lugha iliyotumika katika nathari husika.
(iv)
Wahusika (idadi).
(v)
Dhamira (idadi na uzito).
(vi)
Mandhari (ukubwa na upana-Jiografia,
historia, wakati).
Nathari za Shaaban ni
kama hizi zifuatazo;
15. Adili na Nduguze,
(1952), Mcmillan, Londoni.
16. Kusadikika, (1951),
Nelson, Nairobi.
17. Maisha Yangu na
Baada ya Miaka Hamsini, (1949), Nelson, Nairobi.
18. Kielezo cha Insha,
(1954), Witwatersand, Nairobi.
19. Methali na Mifano
ya Kiswahili, (1997), TUKI, Dar es salaam.
20. Kufikirika, (1968),
Oxford, Nairobi.
21. Utubora Mkulima,
(1968), Nelson, Nairobi.
22. Siku ya Watenzi
Wote, (1967), Nelson, Nairobi.
23. Wasifu wa Siti
binti Saad, (1967), Nelson, Nairobi.
24. Barua za Shaaban
Robert, (2002), TUKI, Dar es salaam.
2.3
UHALISI NA UBUNILIZI KATIKA KAZI ZA SHAABAN ROBERT.
Uhalisi
ni ukweli wa jambo kama lilivyo, kuna ukweli wa aina mbili ambao ni;
(a)
Ukweli katika hali halisi.
(b)
Ukweli wa kisanaa (ambao husawiri mambo
yaliyobuniwa na mtunzi).
Ubunilizi, ni utengenezaji wa ukweli
wa jambo kadri afikiriavyo msanii kwa kuzingatia uwezekano na azma yake. Hivyo
basi yafaa ubunilizi usipitilize kwani ni rahisi kwenda mbali na jamii halisi.
Vipengele ambavyo ubunilizi hufanywa ni kama
vile;
(a)
Mandhari.
Kwa mfano katika kusadikika mandhari iliyotumika ni ya kubuni ambapo tunaona
nchi ya kusadikika iko hewani inaelea, inamipaka sita ambayo ni Ardhini,
Mbinguni, Mashariki, Magharibi, Kusini na Kaskazini.
(b)
Wahusika.
Ambapo wahusika katika kazi za Shaaban Robert wanauwezo na sifa maalumu. Kwa
mfano wanasifa za aina moja tu, kama ni mwema tu au waovu tu. Kama ilivyo kwa
Waziri Majivuno, Karama na kadhalika katika kusadikika. Pia wahusika hawa
huundwa kwa sifa ya kutokukata tama kwa mfano karama katika Kusadikika. Vilevile
wahusika wengine siyo binadamu ni majini kama wanavyojitokeza katika Riwaya
yake ya Adili na Nduguze, kuna wahusika kama vile Mrefu.
(c)
Lugha. Katika kipengele hiki
cha lugha kuna matumizi ya Taswira na tamathali za semi ambapo kwa mwandishi
huyu Shaaban Robert ameonesha umahiri wa hali ya juu katika kipengele hiki,
kuitumia lugha ya Kiswahili.
(d)
Ushikamani,
katika kipengele hiki huweza kufanywa kwa kutumia mbinu kama vile;
(i)
Ubadala mfano katika Adili na Nduguze
hakumtaja sana jina la Mfalme Rai bali alimtambulisha kwa vibadala (majina
mengine ya ziada).
(ii)
Urejeshi/ Kisengere nyuma. Ni ile hali
ya mwandishi kuelezea hadithi Fulani kwa kuanza mbele na kurejea au kulielezea
tukio la nyuma (urejeshi). Kwa mfano msuko wa matukio katika nathari ya
kusadikika.
(iii)
Udondoshaji, katika Adili na Nduguze
mwandishi ameidondosha habari ya mama yao Hasidi, Mwivu na Adili.
(iv)
Uunganishaji/ ujumuishaji. Mfano katika
kusadikika kuna vitushi vya Salii na Sapa, safari za Ndege Mangere na kadhalika
(kitushi ndani ya kitushi).
Hivyo basi kazi za
Shaaban Robert zina mseto wa uhalisi na ubunilizi ambapo kazi zake za mwanzo
zina kiasi kikubwa cha ubunilizi. Mfano Kufikirika, Kusadikika na Adili na
Nduguze. Ambapo ubunilizi huo unajidhihirisha katika kipengele cha Lugha,
Mandhari, Wahusika na namna ya kushikamanisha vitushi vyake ambapo Shaaban
Robert ametumia mbinu mbalimbali kama vile Utomelezi, Taharuki, Ujadi na
kadhalika.
Kazi zake za uzeeni
zina ukweli kwa kiasi kikubwa sana. Kwa mfano Utubora Mkulima na Siku ya
Watenzi Wote.
MBINU
ZA KIBUNILIZI KATIKA KAZI ZA SHAABAN ROBERT NI;
(i)
Ujadi.
(ii)
Ufutuhi.
(iii)
Utomelezi.
(iv)
Taharuki.
(I)
MBINU
YA UJADI
Ni utumizi wa kauli za
Kiutamaduni, kauli zilizozoeleka sana na jamii katika matumizi yao ya kila
siku.
Vipengele vya Ujadi ni
kama vile, methali, misemo, tamathali za semi. Vilevile mtunzi huweza kuiga
kaida maalumu za uzungumzaji ambazo hutumiwa na wazungumzaji wa jamii yake.
Mbinu hii ya ujadi husaidia kumweka mtunzi karibu zaidi na hadhira yake.
(II)
MBINU
YA UFUTUHI
Ufutuhi ni hali
ijengwayo na maneno, matukio au mazingira yoyote yenye mvuto au yasiyo ya
kawaida yenye kuwafanya watu watabasamu au wacheke. (Ponera 2010:6).
Hii ni mbinu ambayo
mtunzi hutumia maneno au hali nyingine inayoweza kusababisha hadhira yake
kupata kicheko/ Ucheshi.
Mfano: Ufutuhi wa majazi katika “Maisha Yangu
na Baada ya Miaka Hamsini”.
Mume ni mume ingawa gumegume
ana sifa ya mtume;
Na mke ni mke ingawa kikwekwe
ana manufaa yake. (uk 101).
Tukio hili
linazungumzia umuhimu wa maisha ya ndoa kwa mwanadamu. Majina ya “Gumegume” na
“Kikwekwe” yanamaanisha sifa za kutokusikiliza na hali ya kukosa utulivu wa
kiakili na kimaadili ya ndoa (Ponera 2010).
(III)
UTOMELEAJI
Ni kitendo cha kuchukua
vipande vya kazi za utanzu mwingine na kuuingiza katika hadithi. Kwa mfano
nathari ya Shaaban Robert ya “Maisha Yangu na Baada ya Miaka Hamsini”,
utomeleaji umejitokeza kwa kiwango cha juu katika ukurasa wa 4-5 katika shairi
la Amina, ukurasa wa 6-20 katika Utenzi wa HATI, ukurasa wa 21-35 Utenzi wa
ADILI. Mbinu hii hutumika ili ku’nogesha kazi yake pia kutia msisitizo juu ya
jambo Fulani.
(IV)
TAHARUKI
Ni hali ya kuwa na
dukuduku la kutaka kujua nini kitafuata katika usimulijia wa hadithi au riwaya.
Mbinu hii mtunzi huitumia ili kuamsha hamu ya msomaji kufatilia kisa kinachosimuliwa
katika riwaya au tamthiliya fulani. Mbinu hii Shaaban Robert ameitumia kama
kijenzi kimojawapo katika utunzi wake. Imejitokeza kwa kiasi kikubwa katika
kazi zake nyingi kama vile “Kufikirika”, ambapo tunaona namna alivyounda
matukio yake kwa namna ya kutia hamasa kuendelea kufuatilia kisa kwa ukaribu
zaidi. Katika Kufikirika tunaona alivyokijenge kisa cha Mfalme na Malkia kuwa
matasa, nathari hii ina muundo ufuatao; Mwanzo, Mfalme, Waganga, Matokeo ya
Utabili, Mtoto wa Mfalme, Kafara, Baraza na Gereza.
3.
MAWAZO AU MTAZAMO WA SHAABAN ROBERT KATIKA MAISHA
Mtazamo ni jinsi ya
kuyatazama au kuyaona mambo na mwelekeo wake. Katika kazi za Shaaban Robert
zinaonesha kuwa mwandishi aliandika kwa kugusia karibu kila Nyanja ya maisha ya
mwanadamu. Baadhi ya mambo hayo ni ukombozi na maendeleo ya nchi, udugu na
familia, mapenzi, dini, umuhimu wa elimu, utu, ujumi wa kiafrika na kadhalika.
3.1.
UTU
Maisha ya binadamu
pasipo utu, hukosa thamani. Baadhi ya maswali yanayoonekana kumshughulisha
Shaaban Robert katika maandiko yake ni kama vile Utu ni nini? Utu hujengwa
wakati gani? na utu hupatikanaje? Utu wa mtu hujengwa na matendo yake mwenyewe
kila siku. Shaaban Robert alilijua vema suala hili na alilichukulia kwa hadhari
kubwa kama asemavyo katika nathari yake;
Hapa Shaaban anasema;
“Wakati mmoja nilifikiri kuwa yote yaliyo azizi au bora kwa mtu ni matendo yake
aliyotenda zamani; na kwa kuwa mimi sikupata kutenda tendo lo lote la maana
nilijiona sawa kabisa na maskini. Wazo hili lilibatilishwa na fikira kuwa
pengine ubora wa mtu huwezekana kuwa katika wakati ujao”. (Maisha Yangu na
Baada ya Miaka Hamsini: uk 1)
3.2 SHAABAN NA DINI
Shaaban Robert alikuwa
Muislamu hivyo aliakikisha pia wote wanaomzunguka pia wanaelekea katika njia ya
kidini, Shaaban aliamini kuwa dini ndio msingi wa amani duniani, mkwa mfano
aliwahusia wanawe kushika dini katika Tenzi zake za HATI na ADILI.
Kwa mfano katika Utenzi
wa HATI anamwambia Mwanjaa na Walimwengu wote kwamba;
27 Shikamana na ibada,
Kutimiza kila muda,
Na kesho ina faida,
Ikisha hii dunia.
28
Dini mali ya roho,
Mwilini kama joho,
Unapoteza uroho,
Na anasa za dunia. (Maisha Yangu na
Baada Ya Miaka Hamsini, uk 10).
Pia katika kitabu
hichohicho ukurasa wa 22 anamuhusia mtoto wake wa kiume Selamani juu ya umuhimu
wa dini katika maisha yake.
Vilevile alisisitiza
uhuru wa kuabudu (Siku ya Watenzi Wote, ukurasa 111), Dhima za dini (Siku ya
Watenzi Wote, ukurasa 16 na 63), Unafiki katika dini (Siku ya Watenzi Wote,
ukurasa 10, 36 na 102). Hivyo basi suala hili kwa Shaaban Robert aliliona ni la
msingi na lenye umuhimu mkubwa katika maisha ya Mwanadamu akiwa hai hapa
duniani.
Pia alitoa maonyo na
maelekezo mengi kwa mdogo wake Yusufu Ulenge juu ya suala hili la dini. Katika
barua yake ya tarehe 24/07/1931 aliyomwandikia Yusufu Ulenge anadhihirisha
hilo. Barua hii ipo katika Barua za Shaaban Robert 1931-1958, barua namba 5
ukurasa wa 32.
3.3
SIASA NA UKOMBOZI
Dhamira halisi ya
Shaaban Robert kupitia maandiko yake haikuupenda ukoloni wala wakoloni wenyewe.
Wahakiki wengi wanamtazama Shaaban Robert kuwa na mawazo ya hali mbili, uchanya
na uhasi kuhusu Ukoloni. Wapo wanomwona kama mpinga ukoloni. Wengine wanamwona
kama alikuwa msaliti/ mwoga juu ya ukoloni.
Katika kazi yake ya
“Utenzi wa Vita vya Uhuru”, tunaona Mawazo ya Shaaban Robert juu ya Ukoloni.
Utenzi huu umezungumzia tukio zima la vita hivyo. Yeye alijiegemeza katika upande
wa Waingereza kama asemavyo bayana katika “Maisha Yangu na Baada ya Miaka Hamsini”
ukurasa wa 64-65. Hapa Shaaban Robert anasema;
“…. Mimi si raia wa Jerumani, ni raia wa
Uingereza…”.
Hili ni mojawapo ya
mambo yaliyozua mjadala kwa wahakiki kuhusu Utanganyika wake, wanadai Shaaban
Robert aliwatukuza wakoloni. Maudhui ya utenzi huu huenda yaliathiriwa na lengo
lake la kumtabarukia Mudir wa Elimu wa kikoloni kipindi hicho Bwana S. N.
Eliufoo.
Mbali na utenzi wa Vita
vya Uhuru, Shaaban Robert amezungumzia ukoloni na siasa katika kazi zake za
“Kusadikika” na “Kufikirika”. Shaaban amefafanua mengi kuhusu adha za Ukoloni
na Wakoloni, kwa mfano katika Tawasifu yake ya “Maisha Yangu na Baada ya Miaka
Hamsini” ukurasa wa 50-51, anaeleza naman alivyobaguliwa yeye na watoto wake
pale aliposhushwa kutoka katika Lori la Abiria cheo cha pili ili kuwapisha
Wahindi waliokuwapo ambao walikosa sehemu ya kukaa kutokana na nafasi katika
Lori hilo kujaa.
SHAABAN
ROBERT NA SUALA LA JINSI NA JINSIA
JINSI,
ni tofauti ya kimaumbile inayojidhihirisha katika via vya uzazi na hivyo
kuwatofautisha watu katika makundi ya wanawake na wanamume.
JINSIA,
ni dhana ya Kisosholojia. Hii inahusu mgawanyiko wa Majukumu baina ya Mwanamke
na Mwanamume.
·
Shaaban Robert amelizungumzia sana jambo
hili katika kazi zake zote. Katika Barua za Shaaban Robert, kuna waraka namba
11.9 katika ukurasa wa 196. Shaaban aliandika Waraka huu kwa Bwana mtengenezaji
katika gazeti la Mambo Leo, aliupa jina la“UKIJUA KUOA NA KUACHA UJUE”’.
·
Vilevile suala hili amelijadili sana
kwenye kitabu chake cha “Wasifu wa Siti Binti Saad”. Siti ameonekana kuwa mfano
mwema wa wake watakiwao Afrika ya Mashariki na Afrika kwa ujumla.
·
Katika nathari yake ya “Kusadikika”,
anasema; “…..hapana haja ya kudharau mwanamke. Wanawake ni Malaika, makao yao
sawa na yale ya pepo…”
·
Pia katika “Maisha Yangu na Baada ya
Miaka Hamsini”, tunamuona jinsi alivyomsifu Amina ukurasa wa 3. Vilevile
anaendelea kumchora kwa kumtetea mwanamke katika ushairi wake. Kwa mfano katika
Utenzi wa HATI katika “Maisha Yangu na Baada ya Miaka Hamsini”, pia na katika
“Pambo la Lugha” katika shairi lisemalo “Mwanamke si Kiatu” (uk 19). Hivyo basi
kwa ujumla maoni na kilio cha Shaaban Robert katika suala hili tunapata katika
kuchunguza kazi zake zote ambapo anawatetea na kuwalalamikia wanaume kuwa ni
watesi na wanyanyasaji wa wanawake. Pia katika maandiko ya Shaaban Robert
hakuna andiko hata moja linalomzungumzia mwanamke vibaya.
3.5
LUGHA
Shaaban Robert katika
kipengele cha lugha anabainika kama Mwalimu na mtetezi wa lugha, hii ni
kutokana na maudhui yanayopatika kutoka katika kazi zake mbalimbali
alizozifanya. Kwa mfano katika kitabu chake cha “Insha na Mashairi”, kuna Insha
mojawapo ya “Lugha ya Tifa” (uk 25). Katika “Siku ya Watenzi Wote” (uk 41)
anasisitiza umuhimu wa mtagusano wa lugha hususani katika kufanya tafsiri.
Pia katika ‘Diwana ya
Almasi za Afrika”, kuna shairi la “Kiswahili 1” na “Kiswahili 2’ (uk 59-60),
pia shairi la “Kitakoma Kiswahili” (uk 65). Vilevile katika barua zake
anajitokeza mara kadhaa kumkosoa Yusufu kuhusu tahajia ya Kiswahili. Katika
kazi hizo Shaaban Robert anajitokeza waziwazi kufundisha, kukemea na
kurekebisha unapotokea upotoshaji wa matumizi ya Kiswahili.
3.6
UJUMI NA KITAMBULISHO CHA MWAFRIKA
Ujumi ni hali/ taaluma
ya masuala ya kutambua uzuri na au ufahamu wa kitu.
Shaaban Robert alikuwa
Mwafrika, aliupenda Uafrika wake na mambo yote yaliyoambatana na hali hiyo.
Ithibati za kuuthamini Uafrika wake inajitokeza katika kazi zake mbalimbali
kama vile;
“Maisha Yangu na Baada
ya Miaka Hamsini” uk 98-100, kupitia utenzi wa ADILI kajitambulisha kuwa yeye
ni Mwafrika. Pia katika uk 50 anasema “…Abiria Waafrika tulikua mimi na watoto
wangu…”
Pia katika “Wasifu wa
Siti Binti Saad” anabainisha utamaduni na Falsafa ya mwafrika wa Kiafrika.
Majina ya Diwani zake
“Almasi za Afrika” na “Mwafrika Aimba”, licha ya majina humo pia kuna mashairi
yasemayo juu ya suala hili. Kama vile “Istaklahi ya Tanganyika” na ‘Fahari ya
nchi yangu”. Hivyo Shaaban Robert ni Mzalendo wa dhati kwani katika kazi zake
anaonesha hilo kwa kutete nchi yake na bara lake, rangi yake, utamaduni wake
(Kiswahili alichokipenda ni sehemu ya utamaduni), Mila na Desturi zake, Vyakula
vya Kiafrika pamoja na Wanawake wa Kiafrika.
3.7
SHAABAN ROBERT NA MAPENZI
Shaaban Robert
amejadili kwa kina mapenzi katika vipengele vya maana halisi ya Mpenzi, aina za
mapenzi, wapi kwa kuyapata mapenzi, mtazamo wake kuhuzu watu wanavyo ya chukulia
mapenzi, faida na hasara za mapenzi.
Mapenzi anayoyajadili
Shaaban Robert ni Pamoja na yale ya Kiumbe kwa Muumba wake, mzazi kwa mtoto au
mtoto kwa mzazi, ndugu kwa ndugu, Ya ndoa, Jamii na Wananchi kwa nchi yao,
Mapenzi ya dhati na ya chati. Katika diwani yake ya “Mapenzi Bora” suala hili
la Mapenzi limejadiliwa kwa undani sana.
Mapenzi ya ndugu kwa
ndugu tunayaona katika nathari ya “Adili na Nduguze”, ambapo Adili alikuwa
akiwapenda sana ndugu zake Mwivu na Hasidi kiasi cha kuwagawia mali zake nusu
kwa nusu pale walipofilisika.
4.0
ITIKADI YA SHAABAN ROBERT
Itikadi ya Shaaban
Robert ni Usoshalisti uliopea, ijapokuwa si katika hali ya kuufikia Ukomunisti.
Itikadi hiyo inasawiri hatua ya juu ya Usoshalisti unaoelekea kwenye Ukomunisti
(Chuachua 2010: 180)
5.0
FALSAFA YA SHAABAN ROBERT.
Shaaban Robert anaamini
kuwa wema hushinda dhidi ya ubaya. Hii inajidhihirisha katika kazi zake nyingi
ambazo mwisho wake huonesha watendewao ubaya huwashinda waovu na kupata haki.
Mfano kama inavyojidhihirisha katika Kusadikika, Kufikirika, Adili na Nduguze
na kadhalika.
6.
MCHANGO WA SHAABAN ROBERT KATIKA FASIHI YA KISWAHILI.
Shaaban ni kiungo dhabiti
baina ya fasihi ya kale na ya sasa. Shaaban Robert ni miongoni mwa waandishi wa
mwanzo katika fasihi ya Kiswahili na waliotumia nguvu kubwa katika uandishi ilikuitoa
fasihi ya Kiswahili sana sana utanzu wa nathari kutoka katika hali ya kihekaya
na kuuingiza utanzu huu ili usawiri maisha halisi ndani ya jamii ya waswahili.
Shaaban Robert ni mmoja
kati ya waasisi wa uandishi wa nathari za kitawasifu katika fasihi ya Kiswahili
kupitia tawasifu yake ya “Maisha Yangu na Baada ya Miaka Hamsini”. Tawasifu hii
yenye sehemu kuu mbili yaani “MAISHA YANGU” na ‘BAADA YA MIAKA HAMSINI”,
inajumla ya kurasa 124. Katika sehemu ya kwanza ya Tawasifu hii (MAISHA YANGU),
imebeba sehemu kumi na tatu (13) ambazo ni Umri, Maisha ya nyumbani, Utenzi wa
Hati, Utenzi wa Adili, Mke wa pili, Idara ya forodha, Uhamisho, Mapumziko, Abiria
cheo cha pili, Idara ya utunzaji wa Wanyama, Naondoka Mpwapwa, Idara ya Utawala
na Nilikuwa mshairi. Sehemu ya pili (BAADA YA MIAKA HAMSINI), inasehemu
zifuatazo Bima, Siasa, Mwandishi, Ukinzani, Kustaafu, Msuso, Upigishaji chapa
na Matukio.
Shaaban Robert, pia ni
mmoja kati ya waandishi waliochangia sana katika maendeleo ya nathari ya Kiswahili. Baadhi ya nathari bunilizi zake
ni; Adili na Nduguze, (1952), Kusadikika, (1951), Maisha Yangu na Baada ya
Miaka Hamsini, (1949), Kielezo cha Insha, (1954), Methali na Mifano ya
Kiswahili, (1997), Kufikirika, (1968), Utubora Mkulima, (1968), Nelson,
Nairobi. Siku ya Watenzi Wote, (1967), Nelson, Nairobi. Wasifu wa Siti binti
Saad, (1967).
Alikuwa na mchango
mkubwa, katika fasihi ya Kiswahili. “Wasifu wa Siti Binti Saad”. Ni moja kati
ya nathari za kwanza kabisa za kiwasifu. Nathari hiyo inaeleza Maisha ya
mwanamuziki mashuhuri wa Taarab Afrika ya Mashariki “Siti Binti Saad”.
Ndiye aliyeizindua
hadhira ya kazi za fasihi ya Kiswahili kuhusu matumizi ya vionjo vya fasihi
simulizi katika fasihi andishi.
Ni miongoni mwa waandishi
wa wakati wake walioandika na kuchapisha kazi nyingi zaidi za fasihi ya
Kiswahili.
HITIMISHO
Shaaban Robetr ni
miongoni mwa wanafasihi waliyoiletea heshima kubwa tasnia ya fasihi ya
Kiswahili. Kazi zao zimekuwa Lulu na mwongozo kwa wanafasihi wanaochipukia
katika uga wa fasihi ya Kiswahili. Msimamo wake wakuwa mwanamapokeo ulikuwa ni
msimamo wa wastani kwani sio wakati wote alizitumia kanuni za kimapokeo,
alizitumia kanuni hizi pale ilipobidi na pale alipotaka kuziacha aliziacha.Vilevile
Shaaban Robert kupitia kazi zake amewasaidia wanazuoni wengi kufikia malengo ya
kielimu, waandishi wakongwe kama E. Kezilahabi ametumia nathari za Shaaban
Robert katika tasnifu yake ya Shahada ya Uzamili.
MAREJEO
Robert, S, (1949),
Maisha Yangu na Baada ya Miaka HamsiniNelson, Nairobi.
(1951),
Kusadikika, Nelson, Nairobi.
(1952),
Adili na Nduguze, Mcmillan, Londoni.
(1954), Kielezo cha Insha, Witwatersand, Nairobi.
(1967),
Siku ya Watenzi Wote, Nelson, Nairobi.
(1967), Wasifu wa Siti binti Saad, Nelson,
Nairobi.
(1968), Kufikirika, Oxford, Nairobi.
(1968),
Utubora Mkulima, Nelson, Nairobi.
(1997), Methali na Mifano ya Kiswahili, TUKI,
Dar es salaam.
(2002),
Barua za Shaaban Robert, TUKI, Dar es salaam.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni